Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 39 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 326 2021-05-28

Name

Dr. David Mathayo David

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Same Magharibi

Primary Question

MHE. JOSEPH A. TADAYO K.n.y. MHE. DKT. DAVID M. DAVID aliuliza:-

Idadi ya watu wa Same imekuwa ikiongezeka tangu tupate Uhuru na mpaka wa Hifadhi ya Taifa Mkomazi upo kilometa tatu kutoka Same Mjini. Wanyamapori na hasa tembo wameonekana Same Mjini mara nyingi.

Je, ni lini Serikali itafikiria kuweka upya mipaka mipya ya hifadhi ili kutoa maeneo kwa ajili ya makazi ya watu na shughuli nyingine za kijamii?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Makao Makuu ya Hifadhi ya Taifa Mkomazi yapo eneo la Zange lililopo umbali wa kilometa sita kutoka Same Mjini. Wanyamapori hususan tembo wanaoonekana karibu na Mji wa Same mara nyingi ni wale wanaotoka katika maeneo ya Ruvu na Simanjiro kuelekea Hifadhi ya Taifa Mkomazi na wale wanaotoka katika Hifadhi ya Taifa Tsavo West nchini Kenya kupitia Ziwa Jipe na Kijiji cha Toloha katika Wilaya ya Same. Ikumbukwe pia kuwa maeneo mengi ambayo wananchi wanaishi kwa sasa yalikuwa yanatumiwa na wanyamapori kama mapito (shoroba) kuelekea maeneo ya Ruvu na Simanjiro.

Mheshimiwa Spika, kuendelea kumega eneo la hifadhi kwa kuweka mpaka mpya wa Hifadhi ya Taifa Mkomazi siyo suluhu ya mgogoro huo kwa sababu eneo hilo litaendelea kuwa makazi na mapito ya wanyamapori. Hata hivyo, katika kudhibiti wanyamapori hao, Serikali itaendelea kuimarisha mikakati inayotumika ambayo ni pamoja na kuendelea kutoa mafunzo kwa wananchi ya mbinu za kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu ambapo mafunzo hayo yanaendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Pia kuimarisha, kuendeleza tafiti na kutumia mbinu mbalimbali za udhibiti na ufuatiliaji wa tembo. Mbinu hizo ni pamoja na mikanda ya elektroniki (collaring) kwa ajili ya kufuatilia makundi ya tembo ambayo ni korofi na kufundisha na kuviwezesha vikundi vya wananchi kwa ajili ya kufuatilia maeneo walipo tembo.

Mheshimiwa Spika, pia matumizi ya ndege zisizokuwa na rubani, matumizi ya pilipili, matumizi ya mizinga ya nyuki na matumizi ya vilipuzi na vifaa vyenye mwanga mkali; lakini pia kutengeneza minara ya kuangalia mbali katika maeneo yanakabiliwa na changamoto ya tembo kuingia. La mwisho ni kuhamasisha wananchi kutoa taarifa mapema pindi wanyamapori ikiwemo tembo wanapoonekana kwenye maeneo ya makazi au mashamba.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa rai kwa wananchi wote wanaoishi katika vijiji vinavyozunguka Hifadhi ya Taifa Mkomazi waendelee kusimamia mipango ya matumizi ya ardhi iliyowekwa pamoja na kushirikiana na Serikali katika kutatua changamoto za wanyamapori wakiwemo tembo pindi zinapojitokeza katika maeneo ya makazi ya watu na shughuli nyingine za kijamii.