Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 37 Energy and Minerals Wizara ya Madini 315 2021-05-26

Name

Ghati Zephania Chomete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. GHATI Z. CHOMETE aliuliza:-

Je, Serikali ina teknolojia gani mbadala ambayo itaepusha kutumia magogo kama matimba kwenye mashimo ya migodi hasa maeneo ya Nyamongo, Tarime, Buhemba na Butiama?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa wachimbaji wengi wadogo nchini na katika maeneo yote yenye shughuli za uchimbaji wa dhahabu yakiwemo maeneo ya Nyamongo, Tarime, Buhemba na Butiama wamekuwa wakitumia magogo na kwa lugha yetu ya kichimbaji yanaitwa matimba na yanatumiwa kama mihimili ulalo pamoja na wima kwenye mashimo ya migodi ili kuweka support. Pamoja na teknolojia hiyo kuonekana kuwa ya gharama nafuu, imekuwa ikisababisha uharibifu mkubwa wa mazingira licha ya kuwa si salama na si ya kudumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, teknolojia mbadala inayotumika kwa sasa ni ujenzi wa mashimo ya migodi kwa kutumia zege pamoja na nondo. Teknolojia hii ni salama na haina athari kubwa za kimazingira ukilinganisha na ile inayotumia magogo. Miongoni mwa sababu zinazopelekea wachimbaji wadogo kutotumia teknolojia hii ni ufinyu wa mitaji, lakini pia, kutokuwa na maeneo ya kudumu ya uchimbaji na baadhi yao kutokuwa na leseni za uchimbaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuwarasimisha wachimbaji wadogo kwa kuwapatia leseni za madini ili waweze kutambulika kisheria na kwa jinsi hiyo kuwawezesha kuaminika katika taasisi mbalimbali za fedha. Aidha, Serikali kupitia STAMICO inaendelea kutoa elimu kwao kuhusu uchimbaji wa kitaalam na wenye tija unaozingatia masuala ya afya, usalama na utunzaji mazingira.