Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 33 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 280 2021-05-21

Name

Irene Alex Ndyamkama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. IRENE A. NDYAMKAMA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakarabati Meli ya Mv. Liemba pamoja na kujenga meli mpya ambazo zitachochea ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Rukwa?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, asante. kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Irene Alex Ndyamkama, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Kampuni ya Huduma za Meli imetenga kiasi cha shilingi bilioni 135 katika mwaka huu wa fedha 2020/2021 kwa ajili ya kutekeleza miradi tisa ya ujenzi wa meli mpya na ukarabati wa meli katika Ziwa Victoria na Tanganyika. Miongoni mwa miradi hiyo ni pamoja na mradi wa ukarabati wa meli ya Mv. Liemba ambayo tayari umeshapata mkandarasi na taratibu za kusaini mkataba zinakamilishwa na itasainiwa mwanzoni mwa mwezi Juni, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na kutekeleza mradi wa ukarabati wa meli ya Mv. Liemba katika Ziwa Tanganyika, Serikali pia imepanga kutekeleza miradi ya ujenzi wa meli mpya ya kubeba abiria 600 na tani 400 za mizigo katika Ziwa Tanganyika, ujenzi wa meli mpya ya kubeba shehena ya mizigo katika Ziwa Tanganyika na ukarabati mkubwa wa meli ya kubeba shehena ya mafuta ya MT. Sangara katika Ziwa Tanganyika. Mikataba ya miradi hiyo ipo katika hatua za mwisho kusainiwa mapema mwanzoni mwa mwezi Juni, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumai yangu kuwa, kukamilika kwa miradi hii kutaondoa adha ya usafiri kwa njia ya maji katika Ziwa Tanganyika na mikoa jirani na Kigoma. Aidha, kutaimarisha na kuifanya nchi yetu kuwa kiungo kikubwa cha soko pana la pamoja linalokisiwa kuwa na idadi ya watu takribani milioni 10 wanaoishi pembezoni mwa ziwa hili katika nchi za Mashariki na Kati ya Afrika ikijumuisha nchi ya Tanzania, Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Burundi na Zambia, ahsante.