Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 31 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 269 2021-05-19

Name

Martha Festo Mariki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARTHA F. MARIKI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuitangaza Hifadhi ya Taifa Katavi?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Festo Mariki, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitekeleza mikakati mbalimbali ya kuitangaza Hifadhi ya Taifa ya Katavi ili iweze kupata watalii wengi na kuongeza mapato. Aidha, Hifadhi ya Taifa Katavi imekuwa ikitangazwa kupitia vyombo vya habari vilivyopo ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kwa kushirikiana na uongozi wa Mkoa wa Katavi iliandaa Mpango Mkakati wa Kukuza Utalii kwa Mkoa wa Katavi mwaka 2019 ambao umesaidia kwa kiwango kikubwa kuitangaza Hifadhi ya hiyo na mikakati mingine inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na Kuvitangaza vivutio vilivyomo ndani ya hifadhi ikiwa ni pamoja na wingi wa Viboko, Simba na Twiga weupe. Vilevile Wizara ina mkakati wa kuitangaza Hifadhi ya Taifa Katavi kupitia tovuti na mitandao ya Kijamii yaani Instagram, Facebook na Twitter lakini pia kuimarisha miundombinu ya barabara ndani ya Hifadhi husika ili kurahisisha kufikika kwa maeneo ya vivutio ndani ya Hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuitangaza Hifadhi hii kupitia chaneli maalum ya Tanzania Safari Channel, lakini pia kusimika mabango kwenye mikoa ya jirani kama vile Mbeya, Songwe, Tabora na Kigoma. Serikali pia inaandaa safari za mafunzo kwa wanahabari, mawakala na wadau mbalimbali wa utalii kwa lengo la kuwapa fursa ya kuvielewa vivutio vya utalii na kuvitangaza ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati mwingine ni pamoja na kujenga sehemu ya malazi ya bei nafuu kwa ajili ya wageni wa ndani na nje ya nchi, na pia kuandaa video au filamu na machapisho mbalimbali na kuyasambaza kwa wananchi na mabasi ili kuitangaza Hifadhi ya Taifa ya Katavi;

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuzitangaza Hifadhi za Taifa kupitia maonesho mbalimbali ya ndani na nje ya nchi ili kuwezesha kupata wawekezaji na watalii. Ni imani ya Serikali kwamba jitihada zinazoendelea kufanywa za kutangaza vivutio hivyo katika Hifadhi ya Taifa ya Katavi zitaendelea kuzaa matunda na hivyo kuwapatia wananchi wa Katavi na Taifa kwa ujumla manufaa stahiki.