Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 31 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 264 2021-05-19

Name

Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Kumekuwa na changamoto ya huduma za Afya katika Zahanati zetu hasa ukosefu wa dawa pamoja na huduma bure kwa wazee, watoto na akinamama wajawazito.

Je, ni lini Serikali itahakikisha Sera ya Afya inatekelezwa bila tatizo lolote?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini kwa kuongeza bajeti ya dawa, vitendanishi na vifaa tiba kutoka shilingi bilioni 31 katika mwaka wa fedha 2015/2016 hadi shilingi bilioni 270 katika mwaka wa fedha 2020/2021. Ongezeko hilo la fedha limewezesha kuongeza upatikanaji wa dawa muhimu (tracer medicine) kutoka wastani wa asilimia 31 mwaka 2015/2016 hadi asilimia 90 kufikia Aprili 30, 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia Mei, 2021 Serikali imetoa huduma ya matibabu bila malipo yenye gharama ya shilingi bilioni 30.1 kwa wananchi wa makundi maalum milioni 12 ikijumlisha wazee, wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi, bado kuna changamoto ya upatikanaji wa baadhi ya dawa za makundi maalum kama wazee, wajawazito na watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano. Ili kukabiliana na changamoto hiyo, mwezi Novemba, 2020 Serikali ilitoa shilingi bilioni 41.2, mwezi Februari, 2021 Serikali ilipeleka shilingi bilioni
18.2 katika vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi kwa ajili ya ununuzi wa dawa na mwezi Mei, 2021 Serikali imepeleka shilingi bilioni 80 na kufanya jumla ya fedha zote zilizopelekwa kwa ajili ya dawa kufikia shilingi bilioni 140.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuboresha upatikanaji wa dawa na bidhaa nyingine za afya ili kuboresha huduma kwa makundi maalum na wananchi kwa ujumla.