Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 30 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 253 2021-05-18

Name

Nancy Hassan Nyalusi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DAVID M. KIHENZILE K.n.y. MHE. NANCY H. NYALUSI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi na kuanza kutumia Hospitali ya Wilaya ya Mufindi?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nancy Hassan Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu katika Hospitali ya Halmashauri. Hadi Aprili 2021, ujenzi wa majengo saba ambayo ni jengo la utawala, jengo la huduma kwa wagonjwa wa nje kwa maana ya OPD, jengo la maabara, jengo la mionzi, jengo la wazazi, jengo la kuhifadhia dawa, jengo la kufulia umekamilika na ujenzi wa wodi ya watoto na wodi ya magonjwa mchanganyiko kwa wanaume na wanawake upo katika hatua ya upandishaji wa ukuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya ya Mufindi. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la upasuaji, jengo la kuhifadhia maiti na wodi ya upasuaji kwa wanaume na wanawake. Hospitali ya Wilaya ya Mufindi imeanza kutoa huduma za wagonjwa wa nje na inatarajiwa ifikapo mwishoni mwa mwaka 2022 hospitali hiyo itaanza kutoa huduma kwa zaidi ya asilimia 90 ya huduma zote zinazotakiwa kutolewa katika ngazi ya Hospitali ya Halmashauri.