Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2015-2020 | Session 2 | sitting 3 | East African Co-operation and International Affairs | Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ushirikiano wa Kikanda na Kimataifa | 33 | 2016-01-28 |
Name
Haji Khatib Kai
Sex
Male
Party
CUF
Constituent
Micheweni
Primary Question
MHE. HAJI KHATIB KAI aliuliza:-
Tanzania ni mwenyeji mkubwa kati ya nchi zilizounda Umoja wa Afrika Mashariki, hivyo basi, hupelekea au hupaswa Watanzania kufaidika na soko la Afrika Mashariki:-
(a) Je, Serikali inawashauri nini wananchi wake wanapokwenda kibiashara kwenye nchi zinazounda umoja huo?
(b) Je, pindi wanapopata matatizo au vikwazo katika nchi husika ni wapi watapeleka malalamiko?
Name
Nape Moses Nnauye
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mtama
Answer
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Haji Khatib Kai, Mbunge wa Micheweni, napenda kutoa maelezo mafupi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zimendoleana ushuru wa forodha mipakani, hatua ambayo inapanua soko la bidhaa za Tanzania kufikia Wanaafrika Mashariki takribani milioni 143 katika nchi tano Wanachama wa Jumuiya za Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi. Hivyo ni dhahiri kuwa, endapo soko hilo litatumika kikamilifu litachangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi wa Taifa na kupunguza umaskini wa wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, sasa napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Serikali inawashauri wananchi kuzichangamkia fursa za kibiashara, ajira, uwekezaji na kadhalika zitokanazo na Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kujiharakishia maendeleo.
Pili, Serikali inawashauri wananchi kuzitambua taratibu za kufuatwa katika kuzitumia fursa za kibiashara zilizopo katika Jumuiya kama nchi wanachama zilivyokubaliana ikiwa ni pamoja na kuwa na cheti kinachobainisha kuwa bidhaa imezalishwa ndani ya Jumuiya yaani cheti cha uasili wa bidhaa- EAC certificate of Origin na vibali/nyaraka kutoka mamlaka husika kutegemeana na aina ya bidhaa mfanyabiashara anazotaka kuuza au kununua.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa katika kufanya biashara katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, vikwazo visivyo vya kiforodha hujitokeza kwa wafanyabiashara wetu kinyume na makubaliano ya nchi wanachama. Napenda kutoa rai kwa wafanyabiashara kuwasiliana na Wizara yangu pindi wanapopata matatizo au vikwazo vya kibiashara katika Jumuiya, Balozi zetu au Vyama vya Wafanyabiashara kama vile Tanzania Chamber of Commerce Industry and Agriculture (TCCIA), Tanzania Private Sector Foundation (TPSF), Tanzania Exporters Assosiation (TANEXA) na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha Wizara imeweka mabango makubwa yani double sided billboards yenye ujumbe wa taratibu za kufuatwa na wafanyabiashara wadogo, wa kati, wa kuuza au kuagiza bidhaa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki katika mipaka ya Horohoro, Rusumo, Kabanga, Namanga, Sirari na Mtukula na vilevile imeweka Maafisa wake katika mipaka ya Rusumo, Mtukula, Namanga na Sirari kwa ajili ya kuwasaidia au kutatua changamoto za wananchi wanapofanya biashara na nchi wanachama.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge kuwahamasisha wananchi katika Majimbo yao kuzitumia fursa zitokanazo na Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa maendeleo ya Taifa kwa ujumla.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved