Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 26 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 221 2021-05-10

Name

Jacqueline Kandidus Ngonyani (Msongozi)

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Lumecha – Londo – Kilosa kwa Mpepo, inayounganisha mkoa wa Ruvuma na Morogoro kwa kiwango cha lami?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Lumecha, Londo, Kilosa kwa Mpepo ni sehemu ya barabara Kuu ya Mikumi, Kidatu, Ifakara, Lupiro, Malinyi Kilosa kwa Mpepo, Londo hadi Lumecha yenye jumla ya kilometa 512 ambayo inaunganisha Mikoa ya Ruvuma na Morogoro. Kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii ulikamilika mwaka 2018 ikiwa ni lengo la Serikali kujenga barabara yote kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi sasa ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Mikumi hadi Kidatu kilometa 35.2 na ujenzi wa Daraja la Magufuli lenye urefu wa mita 384 pamoja na barabara unganishi yenye urefu wa kilometa 9.142 umekamilika. Aidha, ujenzi wa sehemu ya Kidatu – Ifakara ambayo ina urefu wa kilometa 66.9 unaendelea na umefikia asilimia 22.6.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa barabara hii kuanzia Lupilo, Malinyi Kilosa kwa Mpepo, Londo hadi Lumecha, Serikali inaendelea kutafuta fedha za kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami ikiwemo sehemu ya Lumecha, Londo hadi Kilosa kwa Mpepo. Aidha, wakati juhudi za kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami zikiendelea, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania yaani TANROADS Mkoa wa Ruvuma na Morogoro itaendelea kuifanyia matengenezo mbalimbali barabara hii kutoka Ifakara, Lupiro, Malinyi, Kilosa kwa Mpepo, Londo hadi Lumecha kila mwaka ili iweze kupitika majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha huu wa 2020/2021, barabara hii imetengewa jumla ya shilingi milioni 3,610.54 kwa ajili ya matengenezo mbalimbali. Kati ya fedha hizo shilingi milioni 985.585 ni kwa ajili ya sehemu ya barabara ya Lumecha, Londo ambayo iko Mkoa wa Ruvuma, ahsante. (Makofi)