Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 23 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 190 2021-05-05

Name

Abdallah Jafari Chaurembo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbagala

Primary Question

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuipa fedha Halmashauri ya Temeke ili iweze kujenga Shule mpya za kutosha kutokana na Jimbo la Mbagala kuongoza kuwa na wanafunzi wengi wa Shule za Msingi na Sekondari?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Abdallah Chaurembo, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha miundombinu ya elimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke, katika mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2019/2020 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Temeke Shilingi milioni 724 kwa ajili ya ujenzi wa Shule mpya ya Msingi ya Marten Lumbanga na Shule ya Msingi Dovya. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/ 2021 Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kupitia mapato yake ya ndani imejenga jengo la ghorofa moja kwa ajili ya Kidato cha Tano na Sita katika Shule ya Sekondari Mbagala kwa gharama ya shilingi bilioni 1.056.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imeitengea Halmashauri ya Wilaya ya Temeke shilingi bilioni 1.74 ambapo shilingi bilioni 1.53 zitaelekezwa katika Jimbo la Mbagala kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya katika Kata ya Chamazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali ilikamilisha maboma 10 ya madarasa ya Shule za Msingi katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kwa gharama ya Shilingi milioni 137.5. Aidha, kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2019/2020 Serikali imejenga madarasa mapya 25 ya Shule za Msingi katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kwa gharama ya shilingi milioni 500.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2020/ 2021 Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kupitia mapato yake ya ndani imejenga vyumba 76 vya madarasa ya Shule za Sekondari kwa gharama ya shilingi bilioni 1.72. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga Shilingi milioni 220 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba 11 vya madarasa ya Shule za Sekondari katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke. Vilevile, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Shilingi milioni 209 zimetengwa kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya Shule za Sekondari.