Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 22 Good Governance Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 180 2021-05-04

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Vitendo vya rushwa vimekithiri sana katika mchezo wa soka hapa nchini: -

Je, ni kwa kiasi gani Serikali inakabiliana na kudhibiti hali hiyo?

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwepo kwa vitendo vya rushwa katika sekta ya michezo hususan mchezo wa soka hali inayoathiri maendeleo ya mchezo huu kwa ujumla, lakini pia kuikosesha Serikali mapato.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TAKUKURU imekuwa ikikabiliana na vitendo vya rushwa kwenye mchezo wa soka kwa kufanya uchambuzi wa mfumo wa ukusanyaji wa mapato ya viingilio katika mechi za mpira wa miguu. Matokeo ya uchambuzi huo yaliwezesha kubaini kwamba kuna mianya ya rushwa kwenye eneo hili ambapo baada ya kubana mianya hiyo mapato yaliongezeka hadi kufikia shilingi milioni 206 kwa watu 50,233 waliokata tiketi katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa mwezi Machi, 2019 ukilinganisha na mapato ya shilingi milioni 122 kwa watu 47,499 waliokata tiketi kwa mechi iliyochezwa Januari, 2019 kwenye uwanja huo.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa sekta ya michezo nchini, mwaka 2016 TAKUKURU iliunda Timu Maalum ya Uchunguzi kufuatilia na kuchunguza vitendo vya rushwa katika michezo ambapo kesi tatu zimefunguliwa mahakamani na tuhuma saba zinaendelea kuchunguzwa. Aidha, semina zimetolewa kwa makundi mbalimbali ikiwemo Chama cha Makocha wa Mpira wa Miguu (TAFCA), Waamuzi na Makamisaa wanaotumika katika michezo ya Ligi Kuu na Ligi Daraja la Kwanza pamoja na kufanya vikao na viongozi wa Chama cha Mpira wa Miguu (TFF) kuhusu kuweka mikakati ya pamoja kuelimisha umma kupitia soka.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kuwataka TFF, wasimamizi wa soka na viwanja vya michezo waruhusu na kushirikiana na TAKUKURU kuweka matangazo ya kukemea rushwa kwenye soka na michezo kwa ujumla.