Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 17 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 147 2021-04-27

Name

Antipas Zeno Mgungusi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Malinyi

Primary Question

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI aliuliza:-

Sehemu kubwa iliyokuwa ikitumika kwa shughuli za uchumi katika Wilaya ya Malinyi imetwaliwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) mwaka 2017 ambapo waliweka mipaka maarufu kama “TUTA LA 2017” bila kushirikisha wananchi.

Je, Serikali haioni haja ya kurejea na kufanya upya mapitio shirikishi ya mipaka ya eneo hilo?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii napenda kujibu swali la Mheshimiwa Antipas Zeno Mgungusi, Mbunge wa Malinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, maeneo yanayozungumziwa na Mheshimiwa Mbunge ni sehemu ya Pori Tengefu la Kilombero lililoanzishwa mwaka 1952 na kuhuishwa kwa Tangazo la Serikali Na. 269 la mwaka 1974 likiwa na ukubwa wa Kilomita za mraba 6,500. Eneo hilo vile vile ni sehemu ya ardhi oevu yenye umuhimu kitaifa na kimataifa kutokana na kuhifadhi bioanuai mbalimbali na zilizo adimu duniani kama vile mnyama aina ya Puku. Aidha, Bonde hilo huchangia takriban asilimia 62.5 ya maji yote ya Mto Rufiji na hivyo kuwa chanzo muhimu cha maji kwa mradi tarajali wa kufua umeme wa maji wa Julius Nyerere.

Mheshimiwa Spika, aidha tuta linalozungumziwa liliwekwa mwaka 2012 hadi 2013 kwa lengo la kuokoa kiini cha Bonde la Mto Kilombero kutokana na uharibifu mkubwa wa mazingira uliokuwa unaendelea.

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii mwaka 2017 ilifanya mapitio ya mipaka ikiwa ni hatua mojawapo ya kuangalia uwezekano wa kurekebisha mipaka (GN) ili iendane na hali halisi kwani kwa asilimia kubwa eneo la hifadhi lilikuwa limeathiriwa na shughuli za kilimo na ufugaji. Suala hili lilipelekwa kwenye Kamati ya Mawaziri Nane iliyoundwa na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano. Utekelezaji wa mapendekezo hayo umeshafanyika na muda si mrefu wananchi watajulishwa maamuzi ya Kamati hiyo.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa rai kwa Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Wilaya ya Malinyi waendelee kuwa na subira wakati utekelezaji wa maamuzi ya Baraza la Mawaziri ukiendelea kufanyiwa kazi, naomba kuwasilisha.