Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 15 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 124 2021-04-22

Name

Jafari Chege Wambura

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rorya

Primary Question

MHE. JAFARI W. CHEGE aliuliza:-

Je, ni lini Kituo cha Afya Kinesi kitapandishwa hadhi na kuwa Hospitali kamili kutokana na kituo hicho kuhudumia wananchi zaidi ya vijiji 27 katika Jimbo la Rorya?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, na kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya katika Wilaya ya Rorya katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali ilipatia Halmashauri ya Wilaya ya Rorya shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ambapo tayari ujenzi wa majengo saba ya awali umekamilika na huduma za wagonjwa wa nje zinatolewa.

Mheshimiwa Spika, aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu ambapo tayari Halmashauri imeshazipokea fedha hizo na fedha shilingi milioni 500 zimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba. Vilevile katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Rorya. Hivyo, Serikali haikusudii kupandisha hadhi Kituo cha Afya Kinesi kuwa Hospitali ya Halmashauri kwa kuwa Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Rorya.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Rorya shilingi milioni 900 kwa ajili ya kuboresha Kituo cha Afya Utegi kilichopewa shilingi milioni 500 na Kituo cha Afya Kinesi kilichopewa shilingi milioni 400 ambapo ujenzi na ukarabati wa vituo hivyo umekamilika na huduma za upasuaji zimeanza kutolewa. Aidha, Serikali imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya zahanati katika Halmashauri ya Wilaya ya Rorya.

Mheshimiwa Spika, vilevile katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo kimoja cha afya wilayani Rorya na shilingi milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma matatu ya zahanati.