Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 13 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 109 2021-04-20

Name

Festo Richard Sanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makete

Primary Question

MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuitangaza Hifadhi ya Taifa ya Kitulo ili ifahamike kwa Watalii wa ndani na nje?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Taifa ya Kitulo ilianzishwa kwa GN Na. 279 ya mwaka 2005. Hifadhi hii ina sifa ya kipekee kwa kuwa na jamii mbalimbali za maua na kwa nyakati tofauti Serikali imeendelea kuitangaza hifadhi hii na nyingine ziilizopo hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati iliyopo kwa sasa ni kuendelea kuzitangaza hifadhi zote za Taifa ndani na nje ya nchi ikiwemo Hifadhi ya Taifa ya Kitulo. Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kuzitangaza Hifadhi za Taifa kupitia tovuti na mitandao ya Kijamii (Instagram, Facebook na Twitter) pamoja na kuandaa video na filamu mbalimbali na vilevile kuna kuimarisha miundombinu ya barabara ndani ya hifadhi ili kurahisisha kufikika kwa maeneo ya vivutio ndani ya hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati mwingine ni kuzitangaza hifadhi hizi kupitia chaneli maalum ya “Tanzania Safari Channel”; vile vile kuandaa safari za mafunzo kwa wanahabari, mawakala na wadau mbalimbali wa utalii kwa lengo la kuwapa fursa ya kuvielewa vivutio vya utalii na kuvitangaza ndani na nje ya nchi; kujenga sehemu ya malazi ya bei nafuu kwa ajili ya wageni wa ndani na nje ya nchi; na mkakati mwingine ni kuvutia wawekezaji kujenga kambi za watalii au lodge zenye hadhi za Kimataifa, ambapo maeneo manne ya uwekezaji yamebainishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kuona umuhimu wa maeneo ya uhifadhi, bajeti ya mwaka 2021/2022 pamoja na masuala mengine, imezingatia uimarishaji wa utangazaji wa utalii na kuboresha miundombinu ikiwemo barabara, viwanja vya ndege na maeneo ya malazi ya wageni ili kuvutia watalii kutembelea maeneo hayo kwa urahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.