Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 10 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 81 2021-04-15

Name

Ghati Zephania Chomete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. GHATI Z. CHOMETE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Sera ya Matibabu Bure kwa Wazee wenye umri kuanzia miaka 60 katika Halmashauri za Mkoa wa Mara inatekelezeka?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inatekeleza Sera ya Afya ya Mwaka 2007 na Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003, inayoelekeza kutoa matibabu bila malipo kwa wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo kwa kuwatambua na kuwapatia huduma mbalimbali za afya. Hadi Desemba, 2020 jumla ya wazee 2,344,747 wametambuliwa sawa na asimilia ya 87 ya makadirio ya wazee wote nchini. Kati yao wanaume ni 1,092,310 na wanawake 1,252,437. Aidha, wazee wasiokuwa na uwezo 1,087,008 wamepatiwa vitambulisho vya matibabu bure na wazee 856,052 wamepatiwa kadi za matibabu ya Afya ya Jamii (ICHF).

Mheshimiwa Spika, hadi Februari, 2021 Halmashauri za Mkoa wa Mara zimefanya utambuzi wa wazee 70,170 kati ya lengo la kuwatambua wazee 196,000. Kati ya wazee waliotambuliwa, wanaume ni 32,900 na wanawake ni 37,270. Wazee 39,664 wamepewa vitambulisho vya matibabu kati ya wazee 70,170 waliotambuliwa.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Mara na Mikoa mingine inaendelea kufanya utambuzi kwa wazee na kuhakikisha wazee wote wanaotambuliwa wanapewa vitambulisho vya matibabu bila malipo. Aidha, Serikali itaendelea kuwatambua wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo ili waweze kunufaika na Sera ya Matibabu Bila Malipo.