Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 9 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 76 2021-04-14

Name

Nicholaus George Ngassa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa eneo la Hifadhi ya Bonde la Wembere kwa Wananchi wa Igunga kwa ajili ya kufanya shughuli za kilimo na ufugaji ili kumaliza mgogoro wa muda mrefu katika eneo hilo kwa kuwa Bonde hilo limepoteza sifa ya kuwa Hifadhi?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicholaus George Ngassa, Mbunge wa Jimbo la Igunga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Bonde la Wembere ni ardhi oevu inayofahamika Kitaifa na Kimataifa kwa kuhifadhi ndege wa aina mbalimbali ambao huishi na kuzaliana kwa wingi. Eneo hili ni dakio na chujio la maji ya Ziwa Kitangiri na Eyasi, pia ni mapito, mazalia na malisho ya wanyamapori linalounganisha mifumo ya ikolojia ya ukanda wa Kaskazini, Kati, Magharibi na Kusini mwa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na umuhimu wa eneo hilo, wananchi wameendelea kuvamia eneo la ardhi oevu la Wembere kwa ajili ya shughuli za kilimo, malisho na ukataji miti. Hali hiyo inasababisha mwingiliano wa shughuli hizo na kusababisha migogoro kati ya wakulima, wafugaji na wahifadhi. Pamoja na uvamizi huo, eneo hilo bado lina umuhimu katika shughuli za uhifadhi hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa eneo hili la ardhi oevu la Bonde la Wembere na kwa kuzingatia kuwa ni chanzo muhimu cha maji kwa wananchi wa mikoa ya Tabora, Singida na Simiyu, Serikali itafanya tathmini na kutambua mipaka ya ardhi oevu kwa njia shirikishi ya wananchi na Serikali. Na lengo ni kupanga matumizi ya ardhi kwa vijiji vinavyopakana na eneo hilo kwa ajili ya matumizi ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamuomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kutoa ushirikiano kwa Serikali na wananchi katika kushughulikia suala hili ili kupata suluhisho la kudumu. Naomba kuwasilisha.