Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 3 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 35 2021-09-02

Name

Capt. Abbas Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Fuoni

Primary Question

MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI Aliuliza:-

(a) Je, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ina Taasisi ngapi na zipi zina uwezo wa kujiendesha zenyewe?

(b) Je, ni zipi kati ya Taasisi hizo zinapeleka gawio Serikalini?

(c) Je, gawio ni takwa la kisheria?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu Swali la Mheshimiwa Captain Abbas Ali Hassan, Mbunge wa Fuoni lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi inasimamia jumla ya Taasisi 25, kati ya hizo, Mamlaka za udhibiti zipo nne, Taasisi za Utendaji zipo 14, Bodi za Usajili wa Kitaalamu zipo tatu, Vyuo vya Mafunzo ya Kisekta viwili, na Mabaraza ya Walaji ni mawili. Aidha, kuna Vyuo vya Mafunzo ya Kisekta vinne vinavyosimamiwa moja kwa moja na taasisi za kiutendaji. Kati ya hizo, jumla ya taasisi saba zinajitegemea. Taasisi hizo ni TASAC, TCAA, LATRA, TPA, SINOTASHIP, KADCO na CRB.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali ni mmiliki katika Taasisi na Mashirika ya Umma kwa kuwa imewekeza kiasi kikubwa cha fedha. Umiliki wa hisa unatofautiana kulingana na kiasi cha mtaji kilichowekezwa. Kuna taasisi zinamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100 na nyingine chini ya hapo.

Mheshimiwa Spika, mchango hutolewa kwa mujibu wa Sheria ya Fedha, Sura Na. 348 ambayo inataka taasisi ambazo shughuli zake zinahusisha kukusanya maduhuli ya Serikali, kutoa asilimia 15 ya makusanyo ghafi kwa mwaka kama mchango wake katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Aidha, Mashirika ambayo hufanya biashara na Serikali ni mwanahisa mwenza, yanapaswa kutoa gawio kwa serikali kama mbia katika biashara hiyo. Taasisi zote zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi isipokuwa TAZARA na SINOTASHIP zinamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100. Taasisi hizi mbili ndizo zinapaswa kutoa gawio Serikalini na zilizobaki zinatakiwa kutoa mchango kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Hata hivyo, kutokana na utendaji usioridhisha, TAZARA imekuwa haitoi gawio la asilimia 50 inayopaswa kutolewa kwa Serikali ya Tanzania. SINOTASHIP ambayo Serikali inamiliki asilimia 50 imekuwa inatoa gawio Serikalini.

Aidha, Taasisi nyingine zilizobaki chini ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi zimekuwa zinatoa michango yao kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Taasisi ambazo zimekuwa zinakusanya maduhuli na kutoa asilimia 15 ya mapato yao ghafi kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali ni pamoja na LATRA, TASAC, TCAA, TPA, TAA na KADCO. Taasisi zilizobaki hazizalishi mapato na nyingine zimekuwa zinapata ruzuku kutoka Serikalini.

(c) Mheshimiwa Spika, suala la utaratibu wa matumizi na mgawanyo wa gawio na michango ni la kisheria. Suala la gawio limeainishwa kwenye Sheria ya Makampuni Sura Na. 212 ambapo faida inayopatikana baada ya kutoa matumizi yote, Serikali hupata gawio kulingana na kiwango cha hisa kilicho kwenye Kampuni au Taasisi husika. Ahsante.

Mheshimiwa Spika, ahsante.(Makofi)