Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2015-2020 | Session 2 | sitting 3 | Regional Administration and Local Government Authorities | Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa | 30 | 2016-01-28 |
Name
David Ernest Silinde
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Tunduma
Primary Question
MHE. DAVID E. SILINDE aliuliza:-
Wilaya ya Momba ni moja kati ya Wilaya mpya zilizoanzishwa hivi karibuni ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi:-
Je, kwa nini Serikali imekuwa ikisuasua kutoa fedha ili ziweze kujenga ofisi na nyumba za watumishi katika Makao Makuu ya Wilaya ya Momba eneo la Chitete?
Name
Selemani Said Jafo
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kisarawe
Answer
NAIBU WAZIRI WA TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2013/2014, ilifanikiwa kupeleka fedha shilingi milioni 250; ambazo zimetumika kuanza ujenzi wa nyumba ya Mkuu wa Wilaya na ujenzi wa nyumba mbili za Viongozi waandamizi ambao umefikia hatua ya msingi. Katika mwaka wa fedha 2014/2015 fedha zilizotengwa kwa kazi hizo hazikupelekwa. Aidha, katika mwaka 2015/2016, Serikali imetenga shilingi milioni 282.7 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa nyumba hizo na shilingi milioni 200 zimetengwa kuanza ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa ujenzi wa Ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Momba, Serikali katika mwaka wa fedha 2014/2015, ilitoa shilingi milioni 450; kwa ajili ya kuanza ujenzi wa ofisi hizo. Katika jitihada za kuhakikisha Halmashauri inawapatia watumishi wake nyumba bora, Serikali imezielekeza Halmashauri kutumia mapato ya ndani, kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za watumishi. Aidha, Halmashauri imeingia mkata wa ujenzi wa nyumba 20 kwa gharama ya shilingi bilioni 2.1 na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ili kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kujenga nyumba na Ofisi za Viongozi katika Wilaya mpya kwa kadri upatikanaji wa fedha utakavyoruhusu.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved