Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 2 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 20 2021-09-01

Name

Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Primary Question

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa bandari kavu inayojengwa Katosho Kigoma?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kilumbe Shabani Ng’enda, Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Bandari Kavu ya Katosho Kigoma ni kituo kilichosanifiwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kwa ajili ya kuhudumia tani laki tano (500,000) kwa mwaka ili kusaidia kampuni za usafirishaji kuhifadhi makasha kwa muda kabla na baada ya kusafirishwa ndani au nje ya nchi kupitia Bandari ya Kigoma.

Mheshimiwa Spika, kwa hivi sasa upitishaji wa shehena katika bandari ya Kigoma umekuwa ukiongezeka kutoka wastani wa tani 180,000 hadi 200,000 kwa mwaka. Hata hivyo, ongezeko hili la upitishaji wa shehena katika bandari hiyo ni chini ya asilimia 50 ya uwezo uliosanifiwa wa kupitisha tani 700,000 kwa mwaka katika bandari hiyo na hivyo kuifanya bandari Kavu ya Katosho Kigoma kutokuwa na matumizi ya kuweza kusaidia bandari ya Kigoma kwa kuwa bado haijaelemewa katika kuhudumia shehena iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, TPA imekwishalipa fidia wananchi wanaopisha ujenzi wa Bandari Kavu ya Katosho Kigoma yenye ukubwa wa hekta 69 na kazi ya ujenzi wa uzio kwa eneo lote la bandari hiyo imekamilika. Usanifu wa ujenzi wa sakafu ngumu na majengo ya huduma umekamilika na tutaanza kuijenga kwa awamu kuendana na ongezeko la upitishaji wa shehena kuanzia mwaka ujao wa fedha (2022/ 2023). Aidha, uendelezaji wa Bandari Kavu ya Katosho Kigoma upo katika Mpango Kabambe wa TPA kwa mwaka 2009 hadi 2028.