Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 1 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 8 2021-08-31

Name

Mwantatu Mbarak Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Primary Question

MHE. MWANTATU MBARAK KHAMIS Aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwainua Watu Wenye Ulemavu kwa kuwapatia vifaa vya michezo na walimu ili waweze kushiriki mashindano ya kitaifa na kimataifa?

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantatu Mbarak Khamis, Mbunge kutoka Baraza la Wawakilishi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ili kusimamia sekta ya maendeleo ya michezo kwa weledi, Serikali imetengeneza Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Michezo wa Taifa ambao utazinduliwa rasmi mwezi Septemba 2021. Mpango mkakati huo una malengo ya kuendeleza michezo kwa ujumla wake ikiwa ni pamoja na michezo ya watu wenye ulemavu. Mpango huo unaainisha maeneo yote muhimu yakiwemo upatikanaji wa vifaa, ujenzi na ukarabati wa miundombinu, uendelezaji na upatikanaji wa wataalam na walimu wa michezo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na uendelezaji wa mpango huo, Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imekuwa ikiwasaidia wana michezo wenye ulemavu kushiriki katika michezo mbalimbali kwa kuwapatia mahitaji muhimu ikiwa ni pamoja na vifaa vya michezo na wataalam wa mchezo husika. Mathalani mwaka huu wa 2021, Serikali imelipia usafiri, vifaa na posho kwa wachezaji na viongozi wanne kushiriki Michezo ya Paralimpiki inayofanyika nchini Japan – Tokyo kuanzia tarehe 24/08 - 04/ 09/2021. Zaidi ya milioni 15 zimetumika.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2019, Serikali iligharamia timu yetu ya mchezo wa wheel Chair kushiriki mashindano ya Afrika Mashiriki Nairobi Kenya. Mwaka huo huo Serikali iligharamia Timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu kwa watu wenye ulemavu kushiriki mashindano ya Bara la Afrika (CANAF) yaliofanyika nchini Angola. Timu hiyo ilifuzu kushiriki mashindano ya Dunia ya mchezo huo yatakatofanyika mwaka 2022 nchini Uturuki.

Mheshimiwa Spika, kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Michezo uliopo chini ya Baraza la Michezo la Taifa, ni matarajio yetu kuwa tutaendelea kuwasaidia wachezaji wenye ulemavu kwa mahitaji mbalimbali ili waweze kushiriki kikamilifu katika michezo ya Kitaifa na kimataifa kwa kuwapatia maandalizi na kuwa na vifaa mbalimbali pamoja na watalaam pale wanapohitaji msaada huo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.