Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 1 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 3 2021-08-31

Name

Dennis Lazaro Londo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mikumi

Primary Question

MHE. DENNIS L. LONDO Aliuliza: -

(a) Je, ni Watumishi wangapi wamerejeshwa kazini baada ya kuondolewa kimakosa wakati wa zoezi la uhakiki wa vyeti feki na Wafanyakazi hewa?

(b) Je, ni Watumishi wangapi waliorejeshwa kazini wamelipwa stahiki zao kama mishahara ambayo hawakupata kutokana na kuondolewa kazini?

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo, Mbunge wa Mikumi kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia ofisi yangu imewarejesha kazini na kuendelea kuwalipa mishahara jumla ya watumishi 4,380 walioondolewa kwenye orodha ya malipo ya mishahara kimakosa wakati wa zoezi la uhakiki wa vyeti vya elimu na watumishi hewa. Idadi hii inajumuisha Watendaji wa Kata, Watendaji wa Vijiji na Watendaji wa Mitaa wapatao 3,114.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwarejesha watumishi tajwa, Serikali pia ilitoa msamaha wa kuwarejesha kazini watumishi walioondolewa kazini kwa kukosa sifa ya elimu ya Kidato cha Nne na baadaye wakajiendeleza na kupata sifa tajwa hadi kufikia mwezi Disemba, 2020 ambao hawakudanganya katika taarifa zao kuwa wana elimu ya Kidato cha Nne au kubainika kughushi vyeti. Pia, mnamo tarehe 07 Mei, 2021 Serikali kupitia ofisi yangu ilitoa maelekezo na utaratibu kwa waajiri kuhusu namna ya kushughulikia hatima za ajira za watumishi walioondolewa kazini kwa kukosa sifa ya elimu ya Kidato cha Nne pamoja na malipo ya stahiki zao. Napenda kuwakumbusha waajiri wote kukamilisha utekelezaji wa maelekezo hayo kwa haraka na kwa usahihi ili watumishi husika waweze kupata haki zao mapema.

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kusisitiza kwamba msamaha uliotolewa unawahusu watumishi wale tu walioajiriwa baada ya tarehe 20 Mei, 2004 bila sifa ya elimu ya Kidato cha Nne lakini baadaye wakajipatia sifa za kuajiriwa na haiwahusu watumishi waliobainika kuwa na vyeti vya kughushi au waliotoa taarifa za uwongo katika kumbukumbu zao rasmi za kiutumishi. Utaratibu wa kushughulikia watumishi waliobainika kughushi vyeti ulishatolewa awali na Serikali na watumishi wote waliobainika kughushi vyeti hawastahili kurudishwa kazini.

Mheshimiwa Spika, Serikali imelipa madai ya mishahara ya jumla ya shilingi 2,613,978,000 kwa watumishi 1,643 waliorejeshwa kazini baada ya kuondolewa kwenye orodha ya malipo ya mishahara kimakosa. Uhakiki wa madai yaliyobaki unaendelea na yataendelea kulipwa kwa kadri yanavyohakikiwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.