Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 6 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 40 2021-04-09

Name

Dr. Alice Karungi Kaijage

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha inaendelea kuhuisha miundo ya utumishi kwa kada mbalimbali kwa kuwa utaratibu wa kuajiri na kupandisha vyeo ndani ya Utumishi umekuwa ukibadilika kulingana na majukumu ya kiutendaji na maendeleo ya kiuchumi?

Name

Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Answer

WAZIRI WA NCHI OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa kama Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, nimesimama hapa mara nyingi kama Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria kwa kipindi cha tatu sasa cha uenyekiti wangu. Nanze kuchukua fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani kubwa aliyonayo kwangu. Nimuahidi tu kwamba nitakwenda kuchapa kazi kwelikweli, kwenda kupunguza au kumaliza kabisa kero za watumishi wa umma wanyonge ambao ndio msingi wa Taifa letu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili baada ya kumshukuru Mheshimiwa Rais, niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Rufiji, kwa namna moja au nyingine wamekuwa wakiniamini wakati wote waliponichagua mwaka 2015, lakini pia mwaka 2020 nilishinda kwa kishindo kwa kura ambazo hazipata kutokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alice Karungi Kaijage Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa wa Pwani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mujibu wa Kanuni D. 6(2) ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za Mwaka 2009, Watumishi wa Umma huajiriwa na kupandishwa vyeo kwa kuzingatia sifa zilizoainishwa katika Miundo ya Maendeleo ya Utumishi ya Kada husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua mabadiliko ya kiutendaji pamoja na maendeleo ya kiteknolojia na kiuchumi Wizara mbalimbali zimekuwa zikihuisha miundo ya maendeleo ya kiutumishi ya kada mbalimbali zilizo chini yake kwa kuongeza sifa za kielimu, vigezo vya kuajiri na kupandisha vyeo watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa, kwa kutambua mabadiliko ya kiutendaji na maendeleo ya kiteknolojia na kiuchumi, kuanzia mwaka 2014 Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imekuwa ikiziwezesha Wizara Taasisi na Wakala za Serikali kuhuisha miundo yake ya maendeleo ya kiutumishi kadri ya mahitaji mapya yanavyojitokeza. Kwa mfano katika kipindi hicho miundo iliyohuishwa ni pamoja na ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Fedha na Mipango, Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni, pamoja na Taasisi za Umma na Wakala wa Serikali.