Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 5 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 35 2021-04-08

Name

Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Primary Question

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka miundombinu mizuri ya barabara katika Mbuga ya Ibanda na Rumanyika ili kuvutia watalii?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu kwa kuendelea kuniamini kuhudumia Wizara hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hifadhi za Taifa Ibanda-Kyerwa na Rumanyika-Karagwe zilianzishwa kupitia Tangazo la Serikali Na. 509 na 510 la tarehe 05/07/2019. Hifadhi hizo zilitokana na kupandishwa hadhi kwa yaliyokuwa Mapori ya Akiba Ibanda na Rumanyika Orugundu.

Mheshimiwa Spika, katika kuwezesha kufikika kwa hifadhi hizo, Serikali kupitia Taasisi za TANROADS na TARURA imekuwa ikitengeneza barabara mbalimbali zinazorahisisha kufika kwa watalii katika hifadhi hizo. Barabara hizo ni pamoja na Mgakorongo (Karagwe) hadi Murongo (Kyerwa) yenye urefu wa kilometa 112, ambayo inafanyiwa matengezo na TANROADS kila mwaka na imewekwa katika mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami katika Mwaka wa Fedha 2020/2021. Vilevile barabara ya Omushaka – Kaisho – Murongo yenye urefu wa kilometa 120 imekuwa ikifanyiwa matengenezo kila mwaka na TANROADS.

Mheshimiwa Spika, ili kuwezesha uwepo wa miundombinu mizuri ya barabara ndani ya hifadhi, Serikali imetenga shilingi milioni 311.9 kwa mwaka wa fedha 2020/ 2021 kwa ajili ya kuchonga barabara yenye urefu wa kilometa 20 katika Hifadhi ya Taifa Rumanyika-Karagwe. Vilevile, kwa mwaka 2021/2022, Serikali ina mpango wa kutengeneza barabara yenye urefu wa kilometa 51 katika Hifadhi ya Taifa Ibanda-Kyerwa; na barabara ya kilometa 20 katika Hifadhi ya Taifa Rumanyika-Karagwe.

Mheshimiwa Spika, ni imani yetu kwamba jitihada zinazoendelea kufanywa na Serikali za kuboresha miundombinu ya barabara katika Hifadhi za Taifa Ibanda- Kyerwa na Rumanyika-Karagwe na maeneo mengine yote ya hifadhi zitasaidia kuweka mazingira mazuri ambayo yataziwezesha hifadhi hizo kutembelewa na watalii wengi waliopo katika maeneo ya karibu pamoja na wageni kutoka nchi jirani. Naomba kuwasilisha.