Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 2 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 18 2021-03-31

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE Aliuliza: -

Je, ni kwa kiwango gani Serikali inajiridhisha kuwa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu imetolewa kwa wanafunzi walengwa?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Atupele Fredy Mwakibete, Mbunge wa Busekelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inajiridhisha kuwa inatoa mikopo kwa wanafunzi walengwa, kupitia vigezo vilivyowekwa na Sheria ya Bodi ya Mikopo (Sura178) ambayo inawalenga wanafunzi wa Kitanzania wenye sifa za kujiunga na elimu ya juu, lakini kutokana na hali ya kiuchumi hawana uwezo wa kumudu gharama. Vigezo hivyo ni mwombaji anatakiwa awe Mtanzania mhitaji; awe amepata udahili katika taasisi inayotambulika; asiwe na ufadhili wa masomo yake ya elimu ya juu kutoka taasisi nyingine; na awe ameomba mkopo kwa usahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha ili kuwafikia wahitaji wengi zaidi Sheria ya Bodi ya Mikopo imetoa mamlaka kwa Bodi kuweka vigezo vya ziada ambapo katika mwaka wa masomo 2020/2021, Serikali kupitia Bodi ya Mikopo ilitangaza Mwongozo wa Utoaji wa Mikopo uliotaja sifa na vigezo vya ziada kama ifuatavyo: Yatima; mwombaji au mzazi mwenye ulemavu; mwombaji aliyefadhiliwa katika masomo yake ya sekondari au stashahada; na mwombaji aliyetoka katika familia ya kipato cha chini au kaya maskini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia sifa na vigezo hivi, katika mwaka wa masomo 2020/2021, jumla ya waombaji wapya 66,374 wenye sifa za kujiunga na elimu ya juu waliomba mkopo na kati ya hao waombaji 55,318 sawa na 83% walipangiwa mkopo kwa mchanganuo ufuatao: Yatima walikuwa 1,137 sawa na 2.06%; waliofiwa na mzazi mmoja walikuwa 8,683 sawa na 15.7%; waombaji wasiofahamu wazazi au waliolelewa katika Vituo vya Ustawi wa Jamii walikuwa ni 71 sawa na 0.17%; waombaji wenye ulemavu au wenye wazazi wenye ulemavu walikuwa ni 92 sawa na 0.13%; waombaji waliofadhiliwa na taasisi zinazotambulika walikuwa 1,992 sawa na 3.6%); na waombaji kutoka kaya maskini walikuwa 43,343 sawa na 78.35%. Ahsante.