Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 12 2021-03-31

Name

Dr. Christine Gabriel Ishengoma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Hospitali ya kisasa Mkoani Morogoro?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na mpango wa kujenga Hospitali za kisasa za Halmashauri na za Rufaa za Mikoa ili kuboresha huduma za afya za rufaa katika ngazi hizo. Kupitia mpango huo, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro itakarabatiwa na kupanuliwa. Mpango huo utahusika ujenzi wa jengo la kisasa la wagonjwa wa nje, jengo la kutolea huduma za dharura, jengo la huduma za uchunguzi wa mionzi na maabara, matibabu ya viungo, huduma za famasia, utawala pamoja na Wodi Maalum (Private Wards).

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa eneo ilipo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro kwa sasa ni dogo, Serikali kupitia Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro inakamilisha taratibu za umiliki wa eneo lenye ukubwa wa ekari 100 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika kuboresha huduma za afya ngazi ya msingi katika Mkoa wa Morogoro, Serikali imejenga Hospitali tano za Halmashauri ya Malinyi, Gairo, Morogoro, Mvomero na Kilombero kwa gharama ya shilingi bilioni 7.5 katika kipindi cha Juni, 2016 hadi Juni, 2020. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali za Halmashauri ya Mlimba na Mvomero. Aidha, shilingi bilioni 1.5 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa wodi tatu katika Halmashauri za Wilaya za Malinyi, Gairo na Morogoro.