Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 9 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 117 2021-02-12

Name

Deus Clement Sangu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Primary Question

MHE. DEUS C. SANGU Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatatua mgogoro wa ardhi uliopo katika vijiji vinavyozunguka Hifadhi ya Pori la Akiba la Uwanda?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Jimbo la Kwela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Pori la Akiba Uwanda lenye ukubwa wa kilometa za mraba 5,000 lilianzishwa mwaka 1959 na kutangazwa upya kwa Sheria ya Uhifadhi Wanyamapori Na.12 ya mwaka 1974 kwa Tangazo la Serikali Na. 275 la tarehe 8/11/1974. Tangu mwaka 1974 hadi 2013 pori hilo lilikuwa likisimamiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga na lilikabidhiwa rasmi kwa Wizara ya Maliasili na Utalii tarehe 20/01/2014.

Mheshimiwa Naibu Spika, pori hilo linapakana na vijiji 11 kama ifuatavyo; kuna Kijiji cha Ilambo, Kilyamatundu, Mkusi, Kapenta, Maleza, Kilangawana, Mpande, Legeza, Nankanga C, Liwelyamvula na Kipeta; na vijiji saba ambavyo ni Maleza, Kilangawana, Mpande, Legeza, Nankanga C, Liwelyamvula na Kipeta, ndivyo vyenye mgogoro na Pori la Akiba Uwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia mgogoro huo, orodha ya vijiji husika iliwasilishwa kwa Kamati ya Kitaifa ya Migogoro iliyojumuisha Wizara nane. Utekelezaji wa ripoti ya utatuzi wa migogoro ya ardhi ya Mawaziri nane, chini ya Uenyekiti wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, utaleta ufumbuzi wa mgogoro huu na migogoro mingine kama huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi, tunaomba Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Kwela, pamoja na Watanzania wote tuwe na subira wakati utekelezaji wa ufumbuzi wa migogoro hii unaratibiwa. Naomba kuwasilisha.