Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 8 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 113 2021-02-11

Name

Godwin Emmanuel Kunambi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlimba

Primary Question

MHE. NAPE M. NNAUYE K.n.y. MHE. GODWIN E. KUNAMBI Aliuliza: Serikali ina mpango wa kuunganisha mikoa yote kwa mtandao wa barabara za lami, ikiwemo barabara yenye urefu wa kilometa 223 inayounganisha Mikoa ya Njombe na Morogoro kupitia Mlimba ambayo pia iko katika Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM):-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hiyo?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godwin Emmanuel Kunambi, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara anayozungumzia Mheshimiwa Mbunge ni Barabara ya Ifakara – Mlimba – Taweta – Madeke yenye urefu wa kilometa 220.22 ambayo ni barabara ya mkoa inayosimamiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS).

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii imekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa sehemu ya kutoka Ifakara hadi Kihansi (kilometa 126) ili kuunganisha na kipande cha barabara ya lami (kilometa 24) kilichojengwa hapo awali kati ya Kihansi na Mlimba.

Mheshimiwa Spika, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa sehemu iliyosalia kati ya Kihansi na Madeke (kilometa 94.2) umepangwa kufanyika katika mwaka huu wa fedha wa 2020/2021 kwa ufadhili wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB). Kazi hii ipo katika hatua ya manunuzi kwa ajili ya kumpata Mhandisi Mshauri.

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali ina kamilisha usanifu wa kina, imeendelea kutenga fedha na kuifanyia matengenezo mbalimbali barabara hii ili iendelee kupitika kipindi chote cha mwaka ambapo katika mwaka wa fedha 2020/2021, jumla ya shilingi bilioni 2.29 zimetengwa. Ahsante.