Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 5 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 64 2021-02-08

Name

Husna Juma Sekiboko

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kutoa fedha za matumizi mengineyo (OC) kwa Wakuu wa Polisi wa Wilaya kama inavyotoa kwa Wakuu wa vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama?

Name

Khamis Hamza Khamis

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Uzini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nami kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mahali hapa, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwa ametujalia tumekutana hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nichukue fursa hii niwashukuru na kuwapongeza sana wananchi wa Jimbo la Uzini kwa uzalendo na mapenzi makubwa ya kunichagua kwa kura nyingi nikawa Mbunge. Maana wamenitoa kutoka kwenye mavumbi, wamenitoa kwenye majalala, wamenileta kwenye viti, nimekaa na wafalme. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, aidha, nichukue fursa hii nimshukuru na kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, maana baada ya Mungu kuweka baraka, naye ikampendeza akaniteua kuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi. (Makofi)

SPIKA: Sasa jibu swali Mheshimiwa Naibu Waziri. (Makofi/Kicheko)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Husna Sekiboko, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Tanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi kama Taasisi ya Serikali hupokea fedha za matumizi (OC) toka Wizara ya Fedha na huzigawa fedha hizo kupitia Kamati Maalumu ya Fedha (Tanzania Police Force Resources Committee), ambayo huzigawa fedha hizo kwenda kwa Makamanda wa Polisi wa Kanda Maalum, Mikoa na Vikosi; na hao ndiyo wenye mamlaka ya kupata OC kisheria.

Mheshimiwa Spika, jukumu la kugawa fedha kwenda kwa Wakuu wa Polisi wa Wilaya hufanywa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa husika kwa kuzingatia mahitaji halisi ya kila Wilaya, kama vile ukubwa wa wilaya, Idadi ya vyombo vya usafiri ilivyonavyo, ikama ya Askari na takwimu za matukio ya kihalifu yaliyopo. Ahsante.