Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 5 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 61 2021-02-08

Name

Festo Richard Sanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makete

Primary Question

MHE. FESTO R. SANGA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itarudia zoezi la kuweka alama za mipaka kwa kuwashirikisha wananchi ili kumaliza mgogoro uliopo wa mipaka kati ya Hifadhi ya Kitulo na wananchi wa Vijiji vya Misiwa, Makwalanga, Igofi na Nkondo?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mwaka 2016, Serikali ilishaweka alama za mipaka za kati kwenye maeneo ya Hifadhi ya Taifa Kitulo inayopakana na vijiji vya Misiwa, Mwakalanga, Igofi na mwaka 2018 katika Kijiji cha Nkondo.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili la uwekaji wa alama lilishirikisha Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Makete, Waheshimiwa Madiwani, Serikali za Vijiji, wananchi kwa ngazi ya vijiji, pamoja na wataalam wa ardhi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Makete. Elimu ilitolewa kwa wananchi kuhusu zoezi la uwekaji alama za mipaka kwenye vijiji hivi kabla ya uwekaji wa alama za mipaka hiyo. Baada ya utoaji wa elimu, wananchi walichagua wawakilishi watano katika kila kijiji ili kujiunga na timu ya watumishi kutoka Hifadhini na wataalam wa ardhi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Makete, ili kufanya utambuzi wa eneo la mipaka na kuweka mipaka hiyo kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na.279 la Mwaka 2005 la uanzishwaji wa Hifadhi ya Taifa Kitulo.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa taarifa kwamba maeneo hayo tajwa yalikwishawekewa alama za mipaka na zoezi hilo liliwashirikisha wananchi kikamilifu. Lengo kuu la zoezi hilo lilikuwa ni kuhakikisha kuwa mipaka inaonekana bayana na pia shughuli za kibinadamu hazifanyiki ndani ya eneo la hifadhi.

Mheshimiwa Spika, ni imani yetu kwamba mgogoro wa mipaka kati ya Hifadhi ya Taifa Kitulo na vijiji vilivyotajwa ulishapatiwa suluhu kwa kuzingatia Tangazo la Serikali na tunachokiomba kutoka kwa wananchi ni ushirikiano wao ili kuhakikisha kuwa wanashiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi.