Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 4 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 43 2021-02-05

Name

Godwin Emmanuel Kunambi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlimba

Primary Question

MHE. NAPE M. NNAUYE (K.n.y. MHE. GODWIN E. KUNAMBI) aliuliza: -

Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba ni Halmashauri mpya iliyotoka Wilaya ya Kilombero: -

(a) Je, ni lini Serikali itaipa Mlimba hadhi ya kuwa Wilaya hasa ikizingatiwa umbali mrefu wa takriban Km 200 ambao Wananchi wanatembea kufuata huduma Makao Makuu ya Wilaya?

(b) Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa majengo ya Halmashauri na kuboresha miundombinu ya barabara?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godwin Emmanuel Kunambi, Mbunge wa Mlimba lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa miongozo na taratibu, uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala unahusisha uhitaji wa wananchi, Viongozi wa Wilaya na Mkoa ambao huwasilisha maombi ya mapendekezo yao kwenye vikao vya Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) na kisha kuwasilishwa Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa hatua zaidi. Ofisi ya Rais-TAMISEMI, haijapokea maombi rasmi ya Mkoa wa Morogoro kuomba Mlimba kuwa Wilaya. Serikali inashauri utaratibu huu uliowekwa ufuatwe.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 1.1 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba. Mwezi Januari mwaka huu, Serikali imekwisha peleka kiasi cha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuanza shughuli za ujenzi wa jengo hilo la utawala.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa miundombinu ya barabara, katika mwaka wa fedha 2019/ 2020, Serikali imefanya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 54, imejenga kalvati 22 na madaraja manne (4) kwa gharama ya shilingi milioni 545.87. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali kupitia TARURA imetenga kiasi cha shilingi milioni 517.56 kwa ajili ya matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba.