Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 18 2021-02-03

Name

Dr. Charles Stephen Kimei

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vunjo

Primary Question

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI Aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kunakuwepo na Mwongozo kwa Tour Operators wanaopandisha watalii Mlima Kilimanjaro wanaoajiri Wapagazi, Wapishi na Waongoza Misafara kwa kuwalipa ujira stahiki?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nami kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako Tukufu, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii kusimama mbele ya Bunge hili. Vile vile namshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na chama changu kwa kuniamini na leo hii nasimama mbele ya Bunge lako Tukufu.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka 2015 ilitoa Mwongozo kwa Mawakala wa Utalii wa Mlima Kilimanjaro Tour Operators wa kuwalipa ujira stahiki Wapagazi, Wapishi na Waongoza Watalii waliowaajiri kwa ajili ya kuwahudumia watalii wanaopanda Mlima Kilimanjaro.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwongozo huo, Serikali iliagiza kuwa mwongoza watalii alipwe dola za Kimarekani 20 kwa siku, sawa na Sh.40,000 kwa siku, mpishi alipwe dola za Kimarekani 15 sawa na shilingi 30,000 na mpagazi alipwe dola za Kimarekani 10 sawa na Sh.20,000 kwa siku. Wastani wa siku za kupanda mlima hadi kileleni na kushuka ni kuanzia siku 5 hadi 7.

Mheshimiwa Naibu Spika, mnamo tarehe 12 Disemba, 2015, wadau wa utalii wa Mlima Kilimanjaro ambao ni mawakala wa utalii, viongozi wa wawakilishi wa vyama vya waongoza watalii, wapagazi na wapishi walikutana na kusaini mwongozo huo wa malipo ambapo pande zote ziliridhia viwango hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Wizara imeendelea kusimamia utekelezaji wa Mwongozo huu na makubaliano hayo. Katika utekelezaji wa mwongozo, kulijitokeza changamoto ya baadhi ya mawakala wa utalii kutokulipa viwango hivyo na kwa hivyo Serikali iliweka mikakati kadhaa ya kuhakikisha kuwa viwango hivyo vinalipwa kama ilivyoagizwa. Baadhi ya mikakati hiyo ni pamoja na: -

(i) Kushirikiana na Wizara ya Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu kuandaa mikataba ya kisheria ambapo mawakala wa utalii husaini pamoja na waongoza watalii, wapagazi na wapishi wanaoajiriwa kabla ya kuanza kazi. Mkataba huo umeainisha kiwango cha malipo na idadi ya siku atakazofanya kazi na jumla ya malipo anakayostahili kulipwa. Nakala moja ya mkataba huu hukabidhiwa kwenye lango la kupandia mlima, nakala nyingine hupewa waajiriwa (waongoza watalii, wapishi na wapagazi) na nakala moja hubaki kwa wakala wa Utalii.

(ii) Idara ya Kazi imekuwa ikihimiza waajiriwa kutokuanza kazi bila ya kuwa na mikataba. Pia, Idara imekuwa ikifanya ukaguzi wa karibu na wa mara kwa mara katika malango ya hifadhi, ofisi za mawakala wa utalii ili kujiridhisha kuwa utaratibu huo unazingatiwa wakati wote; na

(iii) Changamoto zinazotokana na waajiriwa kutokulipwa kiwango stahiki, kuchelewa kulipwa au kutokulipwa kabisa zimekuwa zikishughulikiwa kwa karibu na Idara ya Kazi na vyama vya waongoza watalii na wapagazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutoa wito kwa waongoza watalii, wapishi na wapagazi kuendelea kujituma katika utekelezaji wa majukumu yao kwa manufaa ya Taifa. Pia, Serikali inaendelea kutoa wito kwa mawakala wote wa utalii kuhakikisha kuwa wanatoa ujira stahiki kwa wahusika ili waendelee kupata motisha ya utendaji kazi.