Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 16 2021-02-03

Name

Cosato David Chumi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. COSATO D. CHUMI Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza Ujenzi wa Barabara za lami na kufunga taa za barabarani katika Mji wa Mafinga chini ya Mpango wa Uendelezaji Miji nchini?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu, kwanza naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia mimi na Waheshimiwa Wabunge wote afya njema na kutuwezesha kuwa wawakilishi wa wananchi kupitia Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa imani kubwa aliyonipa kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Wanging’ombe kwa kunichagua na kuchagua mafiga matatu ya Chama cha Mapinduzi na niwahakishie utumishi uliotukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, naomba sasa kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, nijibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi,Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Miji ya Kimkakati (Tanzania Strategic Cities Projects -TSCP) umetekelezwa katika Halmashauri za Majiji ya Tanga, Dodoma, Mbeya, Arusha na Mwanza na Halmashauri za Manispaa za Mtwara- Mikindani, Ilemela na Kigoma-Ujiji kwa gharama ya Dola za Kimarekani milioni 355.5 sawa na shilingi bilioni 799.52.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Kuendeleza Miundombinu katika Miji 18 (Urban Local Government Strengthening Programme - ULGSP) umetekelezwa katika Halmashauri za Manispaa za Morogoro, Tabora, Moshi, Sumbawanga, Shinyanga, Songea, Iringa, Mpanda, Lindi, Singida, Musoma na Bukoba na Halmashauri za Miji Kibaha, Babati, Geita, Korogwe, Bariadi na Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Miji ya Kimkakati (TSCP) pamoja na Mradi wa Kuendeleza Miundombinu katika Miji 18 (ULGSP) ilimalizika muda wake Mwezi Desemba, 2020. Serikali inaendelea na mazungumzo na Benki ya Dunia kwa ajili ya kuanza kutekeleza Programu nyingine ya kuendeleza miundombinu itakayohusisha Halmashauri26 zilizokuwepo kwenye Programu zilizomalizika pamoja na Halmashauri nyingine 19 za Miji ikiwemo Mafinga.