Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2015-2020 | Session 19 | Sitting 6 | Community Development, Gender and Children | Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto | 48 | 2020-04-08 |
Name
Fatma Hassan Toufiq
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza:-
Elimu ya Afya ya Uzazi ni muhimu sana kwa vijana wa kike na kiume katika kuepuka mimba zisizo za lazima.
Je, Serikali imejipangaje kuwahabarisha vijana ili kupunguza mimba zinazozuilika?
Name
Ummy Ally Mwalimu
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Answer
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau imeaandaa mitaala ya kuwafundishia watumishi wa afya pamoja na vijana kuhusu afya ya uzazi kwa vijana ili kuwajengea uwezo wa kujitambua hasa kuhusu hatua za makuzi wakati wa kubalehe na namna ya kuhimili mihemko ili wasijihusishe na masuala ya ngono katika umri mdogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mafunzo haya huwajengea weledi na stadi za maisha vijana wetu hivyo kuwasaidia kuzingatia masomo zaidi na kujipanga vizuri ili kufikia ndoto zao za maisha. Aidha, Wizara kwa kushirikiana na wadau, mwaka 2018 ilizindua Jukwaa la Vijana la SITETEREKI lenye maudhui mahususi ya kumuelimisha kijana awe na mtazamo chanya wenye kumuwezesha kupata taarifa na huduma muhimu za uhakika kuhusu afya ya Uzazi kwa Vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kwa kushirikiana na Wizara nyingine ikiwemo Wizara ya Elimu pamoja na Wadau wa maendeleo imeandaa Agenda ya Kitaifa ya Afya kwa Vijana na Uwekezaji (NAIA) yenye afua mtambuka zinazowahusu vijana hasa wenye umri wa miaka 10 hadi 19. Ajenda hiyo ilikuwa izinduliwe mwezi Machi mwaka huu, lakini kutokana na tishio la ugonjwa unaotokana na virusi vya Corona zoezi hilo limeahirisha kwa muda.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeona ni vema kuileta mikakati yote inalenga vijana pamoja na kuitengenezea ajenda moja. Ajenda hii imejikita katika maeneo sita ambayo ni eneo la kwanza ni Kuzuia maambukizi ya VVU, eneo la pili ni kuzuia mimba za utotoni na utoro wa shule, eneo la tatu ni Kuzuia unyanyasaji wa jinsia, kimwili na kisaikolojia, eneo la nne ni kuboresha lishe ya vijana; eneo la tano ni kuhakikisha wavulana na wasichana wanabaki shuleni na eneo la sita ni kuwajengea stadi za maisha kupambana na mazingira yanayowazunguka, ni Imani yangu kuwa, tukitekeleza kwa ufanisi afua zilizomo kwenye nguzo hizi tutakuwa tumemwezesha kijana wa Kitanzania kupata elimu ya afya ya uzazi kwa kiasi kikubwa hivyo kuwafanya kuwa rasilimali muhimu katika kuujenga uchumi wa nchi na kuweza kufikia lengo letu la kuwa nchi yenye uchumi wa kati.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved