Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 19 Sitting 5 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 42 2020-04-06

Name

Silvestry Fransis Koka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Mjini

Primary Question

MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-

Mwaka 2000 Serikali kupitia Mradi wa Msitu wa Nishati Ruvu ilitoa leseni ya wakulima zaidi ya 300 kutoka katika Kata za Msangani, Kongowe na Mkuza kulima kwenye hifadhi hiyo.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwamilikisha wakulima hao walioendeleza kilimo kwa takribani miaka 19?

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Msitu wa Hifadhi wa Ruvu Kaskazini umehifadhiwa kisheria kwa Tangazo la Serikali Na. 309 la mwaka 1957. Mwaka 1999/2000 Serikali ikishirikiana na Norwegian Agency for Development Cooperation (NORAD) ilibuni mradi wa kuinua kipato cha wananchi wanaozunguka eneo la Hifadhi ya Msitu wa Ruvu Kaskazini kwa kupitia kilimo mseto ambapo mazao ya chakula pamoja na miti yalipandwa katika eneo moja. Katika kufanikisha hilo, jumla ya wakulima takribani 300 kutoka Kata za Msangani, Mwendapole, Mkuza na Kongowe walipewa eneo la ekari saba kila mmoja kufanya shughuli za kilimo kwa masharti maalum ikiwa ni pamoja na utunzaji misitu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uharibifu uliokithiri pamoja na wakulima wengi kushindwa kutimiza masharti ya leseni walizopewa, mwaka 2015, Serikali iliamua kuachana na utaratibu huo na kuamua kuanzisha mradi mkubwa wa upandaji miti katika eneo husika.

Mheshimiwa Spika, Serikali haina mpango wa kumilikisha sehemu ya msitu huo kwa mtu au taasisi yeyote. Kwa sasa, umefanyika uwekezaji mkubwa wa kupanda miti mbalimbali kibiashara. Kupitia uwekezaji huo, ajira takribani 2,000 zimezalishwa na zinaendelea kuongezeka kufuatia kuanzishwa pia viwanda vya kuchakata mazao ya misitu, hususan bidhaa za mimea ya bamboo.

Aidha, ili kukabiliana na mahitaji ya ardhi kwa wale wenye uhitaji, Serikali inatoa fursa ya kulima kwa mfumo wa kilimo mseto (taungya system), ambapo wakulima wataruhusiwa kulima mazao kwenye maeneo yanayolimwa au kuvunwa miti kwa kibali maalum.