Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 19 Sitting 5 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 41 2020-04-06

Name

Yussuf Salim Hussein

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Chambani

Primary Question

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:-

Je, Tanzania ina Mabwana na Mabibi Misitu wangapi wenye elimu ya Cheti na Diploma?

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein, Mbunge wa Chambani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, taaluma ya Misitu kwa ngazi ya cheti na diploma hapa Tanzania hutolewa na Chuo cha Misitu Olmotonyi kilichopo Arusha. Baada ya uhuru mwaka 1961 hadi 2019, Serikali kupitia Chuo cha Misitu, Olmotonyi imetoa jumla ya wataalam 4,063 wa misitu. Kati ya hao, ngazi ya diploma ni 1,788 wanaume 1,239 na wanawake 549 na katika ngazi ya cheti wataalam ni 2,275 wanaume 1,544 na wanawake 731.

Mheshimiwa Spika, aidha, Chuo cha Viwanda vya Misitu (FITI) kilichopo Mjini Moshi hutoa wataalam wa kusimamia viwanda vya mazao ya misitu katika ngazi ya cheti (astashahada) na diploma (stashahada). Tangu kuanzishwa kwake mwaka 1975, Chuo kimetoa jumla ya wataalam 627, kati ya hao, wangazi ya astashahada ni 510 na stashahada ni 117.

Mheshimiwa Spika, baada ya wahitimu kumaliza masomo yao huajiriwa ama na sekta binafsi, Serikali Kuu, mathalani Wizara ya Maliasili na Utalii na taasisi zake zikiwemo Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Serikali za Mitaa na Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI).

Mheshimiwa Spika, kwa sasa jumla ya Mabwana na Mabibi Misitu 1,227 wenye diploma na cheti wameajiriwa ambapo 770 wapo katika taasisi za Wizara (Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) 748, Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) 16, Chuo cha Misitu Olmotonyi wanne na Chuo cha Viwanda vya Misitu wawili) na 457 wameajiriwa na Serikali za Mitaa. Hata hivyo, ni vigumu kujua kwa usahihi ni wangapi kati ya waliokwishahitimu mafunzo wanaitumikia taaluma yao katika maeneo mbalimbali kutokana na ukweli kwamba baadhi yao wameshastaafu na wengine huenda wanafanya kazi tofauti na taaluma waliyosomea.