Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 19 Sitting 4 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 34 2020-04-03

Name

Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Primary Question

MHE. SAED A. KUBENEA aliuliza:-

Kuna taarifa kwamba ubadhirifu bado unaendelea katika Shirika la NIC; vilevile taarifa zinaonesha kuwa Shirika hilo halina mipango thabiti ya kukabiliana na washindani wake kibiashara:-

(a) Je, ukweli juu ya taarifa hizo ni upi?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuisaidia NIC kifedha na kitaalam ili kuliwezesha shirika hilo kukabiliana na ushindani wa kibiashara?

Name

Dr. Philip Isdor Mpango

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saed Ahmed Kubenea, Mbunge wa Ubungo, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, hakuna ubadhirifu wowote unaoendelea katika Shirika la Bima la Taifa (NIC) na Shirika limeendelea kuboresha mifumo yake ya udhibiti wa mapato na matumizi ili kukabiliana na washindani wake kibiashara katika sekta ya bima. Katika kujiimarisha kibiashara, Shirika limechukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuhakikisha mapato yote yanakusanywa kwa kutumia Mfumo wa Ukusanyaji wa Mapato ya Serikali (GePG) ambao ulianza kutumiwa na Shirika mwezi Novemba 2019 na kuondoa ukusanyaji wa mapato kwa fedha taslimu (cash); kuongeza udhibiti katika ulipaji wa madai ikiwepo kufanya ukaguzi maalum wa madai yote ya Bima za Maisha ili kujiridhisha juu ya uhalali wa madai haya; Shirika lipo katika hatua za mwisho za kuunganishwa na Mfumo wa Usimamizi wa Shughuli za Kihasibu na Malipo katika Taasisi za Umma (MUSE) ambao utaongeza udhibiti katika malipo yote yanayofanyika; kusitisha matumizi ya hundi (cheque) ambapo kuanzia mwezi Desemba 2019, Shirika lilisitisha matumizi ya hundi (cheque) katika malipo yake yote na kuanza kutumia mfumo wa malipo wa kielektroniki hivyo kuongeza uthibiti wa matumizi na kuzuia uwezekano wa matumizi ya hundi feki (forged cheques).

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imechukua hatua mbalimbali kuliimarisha Shirika la Bima la Taifa (NIC) kitaalam kwa kufanya yafuatayo: Kuliondoa Shirika kutoka kwenye mashirika yaliyotakiwa kubinafsishwa na kuliwezesha kushiriki katika biashara ya bima kwa ushindani; imelifanyia mabadiliko ya kiuongozi Shirika ili kuongeza tija na kuleta mabadiliko chanya kwenye utendaji na usimamizi wa shughuli zake; na imelisaidia Shirika kwa kuwapatia wataalamu mbalimbali katika nyanja za mifumo ya TEHAMA, mifumo ya utendaji kazi na mifumo ya utunzaji kumbukumbu (e-Office) ili kuweza kuongeza ufanisi wa Shirika na kuweza kukabiliana na ushindani wa kibiashara.

Mheshimiwa Spika, Serikali pia imeliimarisha Shirika kifedha kwa kuchukua hatua kadhaa ikiwa ni pamoja na kupata biashara za Serikali na kushinikiza malipo ya hapo kwa hapo ya premium ambayo yamesaidia kupunguza malimbikizo ya premium kutoka kwa Taasisi za Serikali kutoka zaidi ya shilingi bilioni 20 hadi milioni 500 kwa kipindi cha Julai 2019 hadi Februari 2020.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maendeleo mazuri ya Shirika, Serikali inaendelea kuliimarisha Shirika hili la kimkakati kwa kulisaidia katika kupitia upya Mpango Mkakati wake ili uendane na mahitaji halisi ya biashara ya ushindani; kuongeza uwekezaji katika mifumo ya TEHAMA ili kuwafikia wateja wengi zaidi; kuongeza ubora wa huduma zake na kulipa madai haraka na kwa urahisi; kujitangaza zaidi na kuongeza uwekezaji wenye tija ili kutoa gawio kubwa kwa Serikali na kushiriki katika shughuli za maendeleo ya Taifa.