Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 19 Sitting 2 Energy and Minerals Wizara ya Madini 18 2020-04-01

Name

Ezekiel Magolyo Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Primary Question

MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-

Kwa kuwa Serikali imekuwa ikiwarasimisha wachimbaji wadogo wa madini:-

(a) Je, ni lini Serikali itawarasimisha Wachimbaji wadogo katika vijiji vya Busulwangili, Lwabakanga, Kakola namba Tisa na Wisolele katika Jimbo la Msalala?

(b) Je, ni sawa kwa mwenye leseni au msimamizi wa eneo la wachimbaji wadogo kupatiwa asilimia 30 ya mawe yanayochimbwa katika eneo lake?

Name

Doto Mashaka Biteko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukombe

Answer

WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tangu mwaka 1996, Serikali kupitia Wizara ya Madini imekuwa ikitenga maeneo maalum kwa ajili ya kurasimisha wachimbaji wadogo wa madini nchini. Hadi sasa, Serikali imetenga jumla ya maeneo 46 katika sehemu mbalimbali nchini yenye ukubwa wa hekta 281,533.69. Aidha, Serikali itaendelea kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo kadri yatakavyokuwa yanapatikana.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Kahama Serikali imeunda Kamati Maalum ya Utengaji wa Maeneo kwa mujibu wa Kifungu cha 15 na 16 cha Sheria ya Madini, Sura 123. Kamati hiyo itakuwa na jukumu la kuandaa utaratibu wa kugawa maeneo yote tengefu yakiwemo maeneo ya Kinamiyuba-Ilindi-Mwime, Buzwagi-Bumbiti na Nyangalata. Mpaka sasa jumla ya maombi 89 ya uchimbaji mdogo yamepokelewa na mchakato wa kugawa leseni hizo unaendelea. Aidha, Serikali kupitia Tume ya Madini imeifuta leseni ya utafutaji wa madini PL 8125/2012 iliyokuwa inamilikiwa na Kampuni ya Liontown Tanzania Limited iliyoko Kata ya Segese Halmashauri ya Msalala na eneo hilo linatarajiwa kutengwa kwa ajili ya wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa maeneo ya Lwabakanga na Kakola namba Tisa aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge, yapo ndani ya leseni ya uchimbaji mkubwa SML 44/99 inayomilikiwa na mgodi wa Bulyanhulu Gold Mine Limited. Hivyo, eneo hilo haliwezi kutengwa kwa ajili ya shughuli za uchimbaji mdogo. Aidha, eneo la Busulwangili lipo ndani ya leseni ya utafutaji wa madini PL 10782/2016 inayomilikiwa na Kampuni ya Hai Nan Geology (Tanzania) Company Limited. Hivyo, Serikali ipo katika hatua za awali za kufuta eneo hilo na kulitenga kwa ajili ya wachimbaji wadogo baada ya mmiliki wake kushindwa kufanya kazi ya utafiti.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Tume ya Madini ilitoa waraka wa ndani Na.3 ulioanza kutumika tarehe 15 Oktoba, 2019, wenye dhumuni la kutoa mwongozo kwa Maafisa Madini Wakazi na watumishi wengine katika kusimamia, kudhibiti shughuli za madini na mapato ya Serikali katika maeneo yenye rush. Waraka huo unawataka wasimamizi kuzingatia ukusanyaji wa kodi za Serikali Kuu na Halmashauri na kuweka mgawanyo wa mapato baina ya mmiliki wa duara (mchimbaji), mmiliki wa shamba na msimamizi. Aidha, kwa Mujibu wa Waraka huo mgawanyo utazingatia kodi za Serikali Kuu na Halmashauri kwanza ambazo ni mrabaha 6%, ada ya ukaguzi 1% na kodi ya huduma 0.3%. Baada ya kutolewa kodi hizo, mmiliki wa ardhi atapata 15%, mmiliki wa shamba 15% na mmiliki wa duara (mchimbaji) 70%.