Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 19 Sitting 2 Good Governance Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 14 2020-04-01

Name

Joram Ismael Hongoli

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Primary Question

MHE. JORAM I. HONGOLI aliuliza:-

Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini umesaidia kuboresha hali za maisha ya Watanzania, hata hivyo baadhi ya Kaya Maskini hazikuingizwa kwenye Mpango huo:-

Je, ni lini Serikali itaingiza Kaya zote katika Mpango huo?

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joram Ismael Hongoli, Mbunge wa Lupembe kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, Kipindi cha Kwanza cha Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini kilitekelezwa kwa miaka sita (6) kuanzia mwaka 2013 hadi 2019. Rasilimali zilizokuwepo zilitosheleza kufikia vijiji/mitaa/shehia 9,960 sawa na asilimia 70. Katika Kipindi hiki jumla ya Vijiji/Mitaa na Shehia 5,590 nchini kote hazikufikiwa.

Mheshimiwa Spika, Ninapenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Kipindi cha Pili cha Mpango huu kimezinduliwa rasmi tarehe 17 Februari, 2020 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Wakati wa uzinduzi wa Kipindi cha Pili, Mheshimiwa Rais aliagiza kufanyika kwa uhakiki wa walengwa wenye sifa za kuwemo kwenye Mpango huo, kuhakikisha kaya zote zenye watu wenye uwezo wa kufanya kazi wanafanya kazi na kulipwa ujira katika miradi ya kuboresha miundombinu ya afya, elimu na maji na kutoa elimu kwa walengwa ili kutumia ruzuku wanazopata kujikita katika kuzalisha na hatimaye kuacha kutegemea ruzuku. Hivyo, utekelezaji wa Mpango huu utaanza rasmi mara baada ya kutekelezwa kwa maagizo hayo.

Mheshimiwa Spika, Kipindi cha Pili cha Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini kitatekelezwa katika halmashauri zote 185 za Tanzania Bara na wilaya zote za Zanzibar katika vijiji, mitaa na shehia zote ikiwa ni pamoja na zile ambazo hazikufikiwa katika Kipindi cha Kwanza; taratibu za utekelezaji wa Kipindi cha Pili zimeboreshwa ili kuwa na walengwa wanaostahili.

Mheshimiwa Spika, aidha, kabla ya kuanza utekelezaji, Serikali itafanya tathmini ya hali ya maisha ya walengwa waliokuwemo katika kipindi cha kwanza cha Mpango huu ili kubaini kaya zilizoimarika kiuchumi na kuziondoa katika orodha ya wanufaika wa ruzuku katika kipindi cha pili. Utaratibu huu umebuniwa kwa lengo la kulinda mafanikio yao ili ruzuku kwa kaya hizi itakapositishwa wasirudi tena katika hali ya umaskini ndani ya kipindi kifupi. Utaratibu uliobuniwa ni kuipatia kila kaya mafunzo ya kuweka akiba na kuwekeza pamoja na kuwapatia mitaji ya kuanzisha shughuli za ujasiriamali kulingana na eneo ambalo wana uzoefu nalo.