Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 53 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 462 2019-06-26

Name

George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Primary Question

MHE. GEORGE M. LUBELEJE aliuliza:-

Serikali ilikuwa na Mpango wa kuifanyia matengenezo makubwa barabara ya kutoka Mima kwenda Mkanana hadi Chibwegele, Mpango huo haujatekelezwa mpaka sasa.

Je, ni lini Serikali itatekeleza Mpango huo ili barabara hiyo iweze kupitika wakati wote bila matatizo kuliko ilivyo sasa?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Malima Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mima hadi Mkanana yenye urefu wa kilomita 23 inaunganisha Kijiji cha Mkanana kilichopo Uwanda wa Mlimani na barabara ya Wilaya iitwayo Gulwe, Chitope inayoambaa uwanda wa chini wa safu za mlima. Barabara hii inahitaji matengenezo makubwa ya kuwekewa tabaka la zege katika sehemu yenye miamba na mlima kwa urefu wa kilomita tano, changarawe kwenye maeneo ya tambarare na ujenzi wa vivuko.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 99 kwa ajili ya kufanya matengenezo makubwa ya barabara ya Gulwe - Chitope yenye urefu wa kilomita 58.8 ambayo inaunganisha barabara ya Mima - Mkanana hadi Chibwegele, Makao Makuu ya Wilaya na Barabara kuu ya Iringa - Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa barabara ya Mima - Mkanana inafanyiwa matengenezo kwenye maeneo korofi kwa urefu wa kilomita tano kwa gharama ya shilingi milioni 42. TARURA imefanya tathmini ya kuikarabati barabara hiyo na kubaini kuwa kiasi cha shilingi bilioni 1.6 zinahitajika ili iweze kupitika katika nyakati zote. Hivyo, Serikali inaendelea kutafuta kiasi hicho cha fedha ili kuiwezesha TARURA kukamilisha kazi hiyo.