Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 52 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 451 2019-06-25

Name

Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Primary Question

MHE. OTHMAN OMAR HAJI aliuliza:-

Lengo kuu la Mpango wa Kujithathmini Kiutawala Bora Barani Afrika (APRM) ni kuziwezesha nchi za Afrika kuimarisha utawala bora kwa kuwawezesha wananchi wake kubainisha changamoto:-

Je, ni hatua gani ambazo zinachukuliwa na Tanzania katika kutekeleza mpango huo?

Name

Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Tanzania ni miongoni mwa nchi 38 kati ya nchi 54 Barani Afrika zinazoshiriki katika Mpango wa Kujitathmini Kiutawala Bora Barani Afrika (APRM) ambapo ilijiunga mwaka 2004 na Bunge la Tanzania liliridhia makubaliano hayo mwaka 2005. Hii ni kutokana na imani kubwa iliyonayo katika lengo kuu la Mpango wa APRM ambalo ni kuziwezesha nchi za Kiafrika kujitathmini kwa vigezo vinavyokubalika vya utawala bora.

Mheshimiwa Spika, matokeo ya tathmini hizo ni kubaini changamoto zilizopo ili ziwekewe mikakati ya kugeuzwa kuwa fursa za maendeleo na pia kubaini maeneo ambayo nchi inafanya vizuri ili kuyaimarisha pamoja na kuigwa mataifa mengine. Tathmini hiyo hufanywa katika maeneo ya siasa na demokrasia, usimamizi wa uchumi, uendeshaji wa mashirika ya biashara na maendeleo ya jamii.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ilikabidhiwa jukumu la kuwezesha utekelezaji wa APRM hapa Tanzania. Katika kutekeleza jukumu hilo, Wizara iliandaa semina na uhamasishaji juu ya Mpango wa APRM ili kuwaandaa wananchi kushiriki kikamilifu katika mpango huo na pia kuwawezesha kuchagua Wajumbe watakaowakilisha makundi yao katika Baraza la Usimamizi la Taifa. Hivyo, mwaka 2006 Wizara iliwezesha kuundwa kwa Baraza la Usimamizi la Taifa lenye Wajumbe 20 kutoka kwenye taasisi za Serikali na taasisi zisizo za Kiserikali.

Mheshimiwa Spika, jukumu kubwa la Baraza ni kusimamia utekelezaji wa shughuli za mpango na kuhakikisha kuwa zinafanyika kwa uwazi, uadilifu na zisiingiliwe kisiasa. Kwa kushirikiana na Wizara, Baraza liliajiri Sekretarieti inayofanya shughuli za APRM za kila siku na taasisi nne za kufanya utafiti katika kila eneo la tathmini.

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwaka 2019, APRM imekwishaandaa taarifa mbili za utawala bora, taarifa ya ndani ya nchi na taarifa ya nje ya nchi. Pamoja na taarifa hizo, umeandaliwa mpango kazi wa APRM wenye lengo la kutatua changamoto za utawala bora zilizobainishwa kwenye taarifa zilizotajwa.

Mheshimiwa Spika, ili kuwezesha utekelezaji wa taarifa za APRM kimeundwa kikosi kazi cha APRM chenye jukumu la kuandaa taarifa za utekelezaji wa kila mwaka na taarifa hizo huunganishwa kuwa taarifa moja ya nchi. Serikali imekuwa ikitenga bajeti kwa ajili ya kazi za APRM kila mwaka na kulipa michango yake kwa taasisi hii kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na Wizara na taasisi za Serikali pamoja na sekta binafsi inaendelea kutatua changamoto za utawala bora kama ilivyoelekezwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 na kuainishwa kwenye mpango kazi wa APRM.