Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 50 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 429 2019-06-21

Name

Gimbi Dotto Masaba

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-

Wananchi wa Wilaya ya Itilima, Mkoani Simiyu huvamiwa na kuharibiwu mazao yao na wanyama aina ya tembo na Serikali hutoa fidia kidogo na wakati mwingine kutowafidia kabisa:-

Je, Serikali inatoa ahadi gani kwa wakulima juu ya fidia kwa waathirika wa uvamizi huo?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vinavyoathiriwa na uvamizi wa wanyamapori hasa tembo katika Wilaya ya Itilima ni vile vinavyopatikana na Pori la Akiba Maswa. Kutokana na changamoto hiyo, Wizara huchukua hatua kadhaa ili kunusuru maisha na mali za wananchi. Hatua hizo ni pamoja na kushughulikia matukio ya uvamizi wa tembo kwa haraka iwezekanavyo pindi yanapojitokeza. Aidha, Wizara imeendelea kutoa elimu ya uhifadhi kwa wananchi kuhusu namna ya kujilinda na kuepuka kulima kwenye shoroba na mapito ya wanyamapori.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imekuwa ikitoa kiasi fulani cha fedha kwa wananchi wanaoathirika na matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu ikiwa ni kifuta jasho na kifuta machozi na siyo fidia kwa mujibu wa Kanuni za mwaka 2011. Mfano, katika kipindi cha miaka miwili ya 2016/2017 na 2017/2018 jumla ya Sh.35,614,000 zimelipwa kwa wananchi 336 wa Wilaya ya Itilima.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kwa sasa Wizara imepokea maombi ya malipo ya kifuta jasho na kifuta machozi ya wananchi 238 kutoka katika vijiji 7 vya Nyantungutu, Ndingho, Ngwalali, Pijulu, Mbogo, Mwamtani B, Lungwa na Longalombogo. Wizara inaendelea kuhakiki maombi hayo na itawalipa wananchi baada ya kujiridhisha na hatua za uharibifu na kiwango cha kifuta machozi wanachostahili kulipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kiasi kinacholipwa ni kidogo na Serikali inatambua suala hili ambapo kwa sasa Wizara inafanya mapitio ya sheria na kanuni za uhifadhi wa wanyamapori, moja ya masuala yanayozingatiwa katika mapitio hayo ni suala la kifuta jasho na kifuta machozi.