Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 50 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 421 2019-06-21

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:-

Serikali ina Mkakati gani wa kuhakikisha kuwa watumishi hewa hawapo katika payroll ya Serikali:-

Je, Serikali inadhibiti vipi mishahara ya watumishi wasiostahili kulipwa kama wastaafu, waliofariki, walioacha kazi na waliofukuzwa kazi katika Halmashauri?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHESHIMIWA JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani mwishoni mwa mwaka 2015 kumekuwepo na mkakati madhubuti wa kudhibiti uwepo wa watumishi hewa katika Mfumo wa Malipo ya Mishahara kwa Watumishi wa Umma nchini. Utekelezaji wa mkakati huo ulifanyika kuanzia mwaka 2016 kwa kuendesha zoezi la uhakiki wa vyeti vya watumishi wote waliopo kwenye taasisi zote za Serikali zikiwemo Mamlaka za Serikali za Mitaa. Katika uhakiki huo, watumishi wote ambao hawakuwa na sifa ya kulipwa mishahara waliondolewa mara moja katika Orodha ya Malipo ya Mishahara (Payroll).

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kudhibiti malipo ya mishahara kwa watumishi wasiostahili kulipwa kama vile wastaafu, waliofariki na waliofukuzwa kazi, Serikali imekuwa ikisitisha mara moja malipo ya mishahara ya watumishi wa aina hiyo kupitia Mfumo wa Taarifa za Kiutumishi (Human Capital Management Information System) na Mfumo wa Malipo ya Mishahara (Government Salary Payment Platform) pindi tu wanapokosa sifa ya kuendelea na Utumishi wa Umma. Mifumo hii inatumika katika Taasisi zote za Serikali zikiwemo Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna udhibiti ulivyo hivi sasa na ufuatiliaji unavyofanyika, hakuna mtumishi anayeweza kulipwa mshahara bila kustahili. Aidha, naomba kutoa wito kwa Maafisa Masuuli katika Taasisi zote za Umma kuendelea kusimamia kikamilifu udhibiti wa malipo ya mishahara kupitia mifumo iliyopo.