Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 43 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 361 2019-06-11

Name

Rukia Ahmed Kassim

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RUKIA KASSIM AHMED aliuliza:-

Baadhi ya magereza nchini yamejaa wafungwa na mahabusu ambao ni wakimbizi.

Je, ni lini Serikali itawarejesha wakimbizi hao makwao ili kupunguza msongamano ndani ya magereza yetu?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rukia Kassim Ahmed, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba miongoni mwa wafungwa na mahabusu walioko katika magereza hapa nchini ni raia wa kigeni wakiwemo wakimbizi kutoka nchi za Burudi, DRC na nchi nyingine duniani. Magereza yenye idadi kubwa ya raia wa kigeni yapo Mkoani Kigoma ambapo yana jumla ya wakimbizi 91 kati yao wafungwa 38 na mahabusu 53. Gereza la Kibondo lina wafungwa 22 na mahabusu 31, Gereza la Kasulu lina wafungwa wawili na mahabusu 19, Gereza la Bangwe lina mfungwa mmoja na mahabusu watatu, Gereza la Ilagala lina mfungwa mmoja na Gereza la Kwitengo lina jumla ya wafungwa 12. Wakimbizi ambao wamefungwa gerezani wanarejeshwa katika nchi zao za asili baada ya kumaliza kutumikia vifungo vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaendelea kuwarejesha wakimbizi nchini kwao kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Wahamiaji (IOM) pamoja na nchi ya Burundi. Kuanzia mwezi wa Julai, 2018 hadi Aprili, 2019 jumla ya wakimbizi 31,643 kutoka Burundi walirejeshwa nchini kwao kwa hiyari.

Mheshimiwa Naibu Spika, idadi hiyo imefanya wakimbizi waliorejeshwa nchini mwao tangu zoezi hilo lilivyoanza mwaka 2017 hadi 2019 kufikia 66,148. Aidha, zoezi la kuwarejesha wakimbizi hao nchini kwao kwa hiari ni endelevu.