Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 42 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 352 2019-06-10

Name

Zubeda Hassan Sakuru

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:-

Ongezeko la gharama za nishati nchini hasa umeme na gesi vimesababisha kuwa na ongezeko kubwa la matumizi ya kuni na mkaa.

Je, ni lini Serikali itarasimisha biashara ya mkaa ili kupunguza makali ya maisha hasa kwa Watanzania wenye kipato duni?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zubeda Hassan Sakuru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, biashara ya kuni na mkaa inafanyika kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Misitu pamoja na Tangazo la Serikali Na. 324 la tarehe 14 Agosti, 2016 na Mwongozo wa Uvunaji wa Mazao ya Misitu wa mwaka 2007 uliofanyiwa marekebisho mwaka 2015. Hivyo biashara hii ni rasmi na haina kizuizi chochote kwa mwananchi yeyote, kinachotakiwa ni kufuata sheria na taratibu za kufanya biashara ambazo zimefafanuliwa vyema katika mwongozo wa uvunaji ambao unamtaka kila mvunaji wa miti kwa ajili ya nishati ya kuni na mkaa kuzifuata, kitu ambacho baadhi ya wafanyabiashara na wachoma mkaa hawatimizi.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya taratibu hizi ni pamoja na:-

(i) Kutambua na kutenga maeneo ya misitu kwa ajili ya kutengeneza mkaa.

(ii) Kila anayehusika na shughuli za biashara ya mkaa anatakiwa kusajiliwa na Meneja wa Misitu wa Wilaya na anatakiwa kuwa na leseni.

(iii) Maombi ya usajili na leseni yanapaswa kupelekwa kwa Afisa Misitu wa Wilaya na kujadiliwa na Kamati ya Kusimamia Uvunaji wa Wilaya; na

(iv) Kila mfanyabiashara wa mkaa anapaswa kulipia mrahaba kama ilivyoainishwa katika Jedwali Na. 14 la Sheria ya Misitu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uhaba mkubwa wa nishati ya miti, Serikali inawahamasisha Watanzania na wadau wote kuanzisha mashamba ya miti kwa ajili ya matumizi ya nishati.

Hata hivyo, tunawaomba Waheshimiwa Wabunge kuisaidia Sekta ya Misitu kwa kuhamasisha matumizi ya umeme, gesi, uzalishaji wa nishati mbadala ili kupunguza matumizi ya nishati ya kuni na mkaa ambayo inaongeza uharibifu wa misitu.