Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 40 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 333 2019-05-31

Name

Yussuf Haji Khamis

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Nungwi

Primary Question

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS aliuliza:-

Upimaji wa Afya za Wanamichezo ni jambo muhimu kwa ajili ya kulinda na kuhakikisha afya zao kabla ya kushiriki michezoni kwani kumekuwa na matokeo mbalimbali ya Wanamichezo kupoteza maisha wakiwa uwanjani. Mathalani, Ismael Mirisho wa Timu ya Mbao FC, Marc Vivien Foe wa Cameroon na Cheikh Tiote wa Ivory Coast:-

Je, Serikali kupitia Vyama vya Michezo vimeweka utaratibu gani kuhakikisha upimaji wa afya za wanamichezo ni jambo linalopewa kipaumbele?

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri, wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Haji Khamis, Mbunge wa Nungwi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia na kuwa na uelewa sahihi kuhusu umuhimu wa afya za wachezaji wetu wakiwa michezoni. Matukio ya wanamichezo kupata matatizo ya kiafya na hata wakati mwingine vifo kutokea uwanjani, yamekuwa yakitokea mara kwa mara Tanzania na imeshuhudiwa matukio kama hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia ukweli huo, Wizara yangu kupitia kitengo chake cha Kinga na Tiba kwa kushirikiana na Chama cha Madaktari wa Michezo Nchini, imeendelea kutoa elimu ya afya kwa wanamichezo na Viongozi wa Mashirikisho ya Vyama vya Michezo kwa lengo la kuwawezesha kuelewa umuhimu wa huduma za afya kwa wanamichezo muda wote wawapo viwanjani kwa mazoezini au katika mashindano.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo huo, vilabu vyote vya soka vya ligi kuu ya Tanzania kwa mfano, vimeelekezwa kuwa na Daktari mwenye sifa na ambaye muda wote atakuwa tayari kutoa huduma ya matibabu kwa wachezaji.

Mheshimiwa Spika, Kitengo cha Kinga na Tiba cha Wizara, mbali ya kutoa elimu ya afya kwa wanamichezo pia kina jukumu la upimaji wa afya na kutoa Huduma ya Kwanza kwa wanamichezo kila wanaposhiriki michezo au mashindano mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, suala la huduma za afya kwa wanamichezo ni suala la kisera. Sera ya Maendeleo ya Michezo ya Mwaka 1995 sehemu ya 10.1 imeelekeza kuwa ni lazima mchezaji achunguzwe afya yake na kuwekewa kumbukumbu zote za kiafya kwa kipindi chote awapo kambini na ahudumiwe na Daktari kwenye taaluma ya tiba kwa wanamichezo.

Aidha, utaratibu wa matibabu kwa wanamichezo ujumuishe mafunzo juu ya athari za kutumia madawa ya kuongeza nguvu kwa wanamichezo. Wizara yangu inashauri na kuelekeza Vyama na Mashirikisho yote ya Michezo Nchini kuwa na utaratibu wa mara kwa mara wa kutoa elimu ya afya kwa wadau wake pamoja na kutoa elimu kinga kwa wanamichezo ili kulinda afya zao. Wizara yangu iko tayari kutoa ushirikiano katika jitihada hizo kwa kutoa ushauri wa kitaalamu ili kuimarisha afya za wanamichezo.