Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 39 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 329 2019-05-30

Name

Jaku Hashim Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Primary Question

MHE. MACHANO OTHMAN SAID (K.n.y. MHE. JAKU HASHIM AYOUB) aliuliza:-

(a) Je, ni lini TRA itakaa na wafanyabiashara wa Tanzania kusikiliza vilio vyao licha ya kila Mkoa unayo Ofisi ya TRA?

(b) Je, ni sababu gani zinazofanya mizigo inayotoka Zambia, Uganda, Kenya, DRC haipati usumbufu inapoingia Jijini Dar es Salaam katika bandari lakini mizigo kutoka Zanzibar inakuwa kero kubwa inapoingia Jiji la Dar es Salaam kupitia bandarini?

(c) Je, ni lini TRA itaweka Ofisi kila Mkoa kusikiliza kero za wafanyabiashara ambao wanahisi wanaonewa na vilevile kuweka Mwanasheria kila Ofisi ili pasiwepo na manung’uniko ya wafanyabishara kuonewa?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashimu Ayoub, Mbunge wa Baraza la Wawakilishi, lenye sehemu (a) (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, miongoni kwa kazi za kila siku za Mamlaka ya Mapato Tanzania ni kusikiliza na kutatua kero za wafanyabiashara ili kuwawezesha kufanyabiashara zao bila usumbufu. Mamlaka ya Mapato Tanzania hufanya mikutano au vikao na wafanyabiashara katika ngazi ya Wilaya, Mikoa na Taifa ili kutoa elimu ya kodi, kusikiliza vilio au kero zao na kuzifanyia kazi; hurusha vipindi maalumu katika televisheni na redio vinavyotoa elimu ya kodi kwa wananchi na kujibu kero za wafanyabiashara; huboresha na kuweka kwenye tovuti ya Mamlaka taarifa mbalimbali za kikodi na pia hubuni na kuanzisha mifumo, vituo na vilabu rafiki vya kikodi ili kujibu vilio vya wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Mapato Tanzania imeanzisha call centre, Makao Makuu Dar es Salaam pamoja na Kituo cha Huduma za Ushauri kwa Mlipakodi kilichopo Somara, Jijini Dar es Salaam ili kutoa fursa kwa wafanyabiashara kuwasilisha maoni na kero za kikodi kwa wakati. Pia, Wenyeviti wa Kamati za Mapato za Mikoa na Wilaya ambao ni Wakuu wa Mikoa na Wilaya wamekuwa wakisilikiza kero za walipakodi katika Mikoa na Wilaya zao na kuzitatufia ufumbuzi kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii, kuwahimiza wananchi kutembelea Ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania zilizopo katika maeneo yao na kuhudhuria vikao vinavyoitishwa na Wakuu wa Mikoa na Wilaya ili kuwasilisha maoni na kero za kikodi.

(b) Mheshimiwa Spika, siyo kweli kwamba bidhaa za Zanzibar zinapata usumbufu ikilinganishwa na bidhaa za nchi jirani zinapoingia Tanzania Bara kwa sababu bidhaa zote zinafuata utaratibu wa forodha unaofanana. Bidhaa zinazoingia Tanzania Bara kutoka nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kupata msamaha wa Ushuru wa Forodha lakini hulipiwa Kodi ya Ongezeko la Thamani pamoja na Ushuru wa Bidhaa.

(c) Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Mapato Tanzania ina Ofisi katika Mikoa yote ya Tanzania pamoja na baadhi ya Wilaya zake. Aidha, baadhi ya Mikoa ina vituo maalum vya huduma za kodi hususani Dar es Salaam, Mwanza, Arusha na Mbeya.

Mheshimiwa Spika, pili, kila Mkoa una Mwanasheria na Afisa Elimu ya Kodi kwa ajili ya kutoa elimu, kusikiliza na kutatua kero za walipakodi. Pia, Mamalaka imeweka utaratibu wa Mameneja wa Mikoa ya kikodi kukutana na walipa kodi kila Alhamisi ili kusikiliza kero zao na kuzitatua. Hatua hii ina nia ya kujenga imani ya walipakodi, kutatua kero na kukuza ridhaa ya ulipaji kodi kwa hiari.