Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 33 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 272 2019-05-22

Name

Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Primary Question

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza:-

Kupitia Sera ya Serikali ya kila kata kuwa na kituo kimoja cha afya, ni kata mbili tu zimebahatika kuwa na vituo vya afya kati ya kata kumi na saba (17) za Halmashauri ya Mji wa Mbulu; vituo hivi viko kwenye Tarafa za Daudi na Endagikot:-

(a) Je, ni lini Serikali itajenga kituo kimoja cha afya Kata za Kainam au Muray kwa ajili ya kupeleka huduma ya afya katika Tarafa ya Nambis yenye kata nne na vijiji ishirini na mbili na wakazi 24,800 kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012?

(b) Serikali ina sera ya kutoa huduma za afya bila malipo kwa watoto walio chini ya miaka mitano na akina mama wajawazito; je, Serikali inachukua hatua gani katika vituo ambavyo bado vimeendelea kuchangisha kundi hili muhimu katika jamii?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya uhaba wa vituo vya afya katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu. Kutokana na hali hiyo, Serikali iliamua kuanza na ujenzi wa Vituo vya Afya viwili na Daudi na Tlawi vilivyogharimu jumla ya shilingi bilioni moja kwa kila kituo kupata shilingi milioni 500. Hata hivyo, Serikali inatambua na imesikia kilio cha Mheshimiwa Mbunge, Serikali itafanya juhudi kwa kadri iwezekanavyo ili kuwasaidia wananchi wa kata hizo.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeongeza bajeti ya dawa kutoka shilingi bilioni 31 hadi bilioni 270 ili kuboresha huduma za afya kwa wananchi yakiwemo makundi yenye msamaha wa matibabu. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imeidhinishiwa jumla ya shilingi bilioni 104 kupitia Mfuko wa Afya wa Pamoja, ile basket fund, ambapo sehemu kubwa ya fedha hizo ni kwa ajili ya dawa na vifaatiba. Hivyo, Serikali haitarajii kuona akina mama wajawazito pamoja na watoto wenye umri chini ya miaka mitano wakichangishwa. Serikali haitasita kuchukua hatua kwa wote watakaobainika kuwatoza makundi hayo kwa kuwa ni kinyume na maelekezo ya Serikali. (Makofi)