Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 8 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 103 2019-09-12

Name

Jaku Hashim Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Primary Question

MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuliza:-

(a) Je, ni lini Benki ya FBME italipa wateja amana zao zilizokuwepo kwenye Benki hiyo?

(b) Je, Benki iko katika hali gani sasa?

(c) Je, Benki Kuu ya Tanzania ina dhamana gani katika kulinda Mabenki?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango na kwa kuzingatia maombi ya Mheshimiwa Jaku, naomba kujibu swali lake lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Benki ya FBME Limited ilifutiwa leseni ya kufanya biashara hapa Tanzania na Benki Kuu ya Tanzania mnamo tarehe 8 Mei, 2017 kutokana na tuhuma za kujihusisha na biashara ya kutakatisha fedha huko nchini Marekani. Aidha, Benki Kuu iliteua Bodi ya Bima ya Amana kuwa Mfilisi wa Benki hiyo. Katika kitimiza wajibu wake wa msingi, Bodi ya Bima ya Amana ilianza zoezi la kulipa fidia kwa mujibu wa Sheria kwa waliokuwa na amana katika benki hiyo kuanzia mwezi Novema, 2017 na bado zoezi hilo linaendelea.

Hadi kufikia tarehe 9 Septemba, 2019 jumla ya kiasi cha shilingi milioni 2,404.2 kimelipwa kwa wateja 3,426 kama fidia ya Bima ya Amana. Kiasi hicho ni sawa na asilimia 55.9 ya kiasi chote kilichotarajiwa kulipwa kama fidia ya Bima ya amana kwa wateja wote 6,628 waliopo Tanzania pamoja na wateja waliopo nje ya nchi (Tanzania International Banking Depositors). Aidha, jumla ya shilingi milioni 2,401.2 zimelipwa ikiwa ni asilimia 83.3 ya lengo la kulipa jumla ya shilingi milioni 2,882.6 kwa wateja waliopo Tanzania tu.

Mheshimiwa Spika, wateja waliokuwa na amana zaidi ya shilingi milioni 1.5 watalipwa kiasi kilichobakia kwa mujibu wa sheria na taratibu za ufilisi. Kiasi kitakacholipwa kwa wenye amana zaidi ya shilingi milioni 1.5 kitategemea fedha zitakazopatikana kutokana na mauzo ya mali za benki pamoja ukusanyaji wa madeni kutoka kwa wadeni wa benki hiyo.

(b) Mheshimiwa Spika, kwa sasa Benki ya FBME Limited ipo katika hatua za ufilisi na hivyo haiendeshi shughuli zozote za kibenki hapa nchini.

(c) Sheria ya Benki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 imeipa Benki Kuu ya Tanzania mamlaka ya kutoa leseni, kutunga Kanuni, kusimamia benki zote zinazochukua amana za wateja na kuchukua hatua za kisheria dhidi ya benki zinazoendesha biashara bila kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo iliyopo.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla, Benki Kuu imepewa mamlaka ya kusimamia na kudhibiti benki na taasisi za fedha ili kuhakikisha kuwa amana za wateja zinakuwa salama pia kuna usalama, utulivu na uthabiti wa Sekta ya Fedha na uchumi kwa ujumla. (Makofi)