Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 8 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 102 2019-09-12

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. ALEX R. GASHAZA (k.n.y. MHE. OSCAR R. MUKASA) aliuliza:-

Mwanzoni mwa mwaka 2016 wananchi wa Kijiji cha Kabukome Kata ya Nyarubungo Wilaya ya Biharamulo walivamiwa na tembo na kupoteza asilimia kubwa ya mazao yao:-

Je, ni lini wananchi hao watapata fidia ya mazao yao?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kufuatia kuongezeka kwa juhudi za uhifadhi nchini na kupungua kwa ujangili, wanyamapori hususan tembo wamekuwa wakitoka ndani ya hifadhi na kupita maeneo ambayo ni shoroba au maeneo ya vijiji yanayopakana na maeneo ya hifadhi, ikiwemo baadhi ya vijiji vinavyopakana na yaliyokuwa mapori ya akiba ya Biharamulo na Burigi, kwa sasa ni Hifadhi ya Taifa ya Burigi - Chato katika Wilaya ya Biharamulo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto hiyo, Wilaya imekuwa ikichukua hatua kadhaa ili kunusuru maisha na mali za wananchi ambazo ni pamoja na kushughulikia matukio ya uvamizi wa wanyama kama tembo kwa haraka ikiwezekana pindi yanapojitokeza na kutoa elimu ya uhifadhi kuhusu namna ya kujilinda, lakini pia wananchi kuepuka kulima kwenye shoroba na mapito ya wanyamapori.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imekuwa ikitoa fedha kama pole kwa wananchi wanaoathirika na matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu ikiwa ni pamoja na kifuta jasho na kifuta machozi, siyo fidia kwa mujibu wa Kanuni ya Kifuta Jasho na Kifuta Machozi ya Mwaka 2011. Aidha, Kanuni husika zinafanyiwa marekebisho ambapo kwa sasa maoni ya wadau ndani na nje yamekusanywa, hatua inayofuata ni kuwasilisha kanuni hizo kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na baada ya hapo zitasainiwa na Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, kumbukumbu zinaonyesha kuwa katika kipindi cha mwaka 2016/2019, Wizara yangu haijapokea maombi yoyote kutoka Kijiji cha Kabukome, Kata ya Nyarubongo, Wilaya ya Biharamulo. Hivyo ninashauri Mheshimiwa Mbunge kupitia Halmashauri ya Wilaya kuwasilisha maombi husika ili yafanyiwe kazi kwa mujibu wa Kanuni za Kifuta Jasho na Kifuta Machozi za Mwaka 2011. Wananchi watakaokidhi vigezo watalipwa kifuta jasho mara baada ya taratibu kumalikika.