Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 70 2019-09-10

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:-

Shule ya Msingi Kambarage ni shule pekee katika Wilaya ya Liwale inayochukua watoto wenye mahitaji maalum (walemavu); lakini shule hiyo haina walimu wenye taaluma hizo na vilevile miundombinu ya shule hiyo sio rafiki kwa watoto wenye ulemavu:-

(a) Je, ni lini shule hiyo itapatiwa walimu wenye taaluma husika ili kukidhi mahitaji ya shule?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mazingira ya shule hiyo ili iweze kukidhi mahitaji ya watoto hao?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuberi Mohamed Kuchauka, Mbunge wa Liwale lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Shule ya Msingi Kambarage ina wanafunzi 1,283 wavulana wakiwa 636 na wasichana 647. Shule inatoa elimu changamani ambapo wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia wapo 10, wenye ulemavu wa akili kwa maana ya mtindio wa ubongo wapo watano na wenye ulemavu wa ngozi wapo watatu. Uwiano wa walimu na mwanafunzi unatofautiana kulingana na aina ya ulemavu wa wanafunzi. Ulemavu wa akili mwalimu mmoja kwa wanafunzi watano, ulemavu wa kusikia mwalimu mmoja kwa wanafunzi tisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shule ya Msingi Kambarage ina walimu watatu wanaofundisha wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia na mwalimu mmoja kwa wenye ulemavu wa akili. Kwa uwiano huo walimu na wanafunzi ni wazi kuwa hakuna upungufu wa walimu kwa wanafunzi kwenye mahitaji maalum katika shule hiyo.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya tathimini ya miundombinu katika Shule ya Msingi Kambarage na kubaini kuwa kiasi cha shilingi milioni 50 kinahitajika kwa ajili ya kujenga na kukarabati miundombinu kwenye Shule ya Msingi Kambarage. Naielekeza Halmashauri ya Wilaya ya Liwale kutenga fedha hizo kwenye bajeti zake zinazotokana na mapato ya ndani kwa ajili ya kufanya ukarabati na ujenzi wa miundombinu.