Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 5 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 59 2019-09-09

Name

Dr. Dalaly Peter Kafumu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-

Asilimia 70 au zaidi ya maeneo ya Kata za Isakamaliwa, Mbutu, Igunga, Nguvumoja, Lugubu na Itumba katika Jimbo la Igunga na Kata za Igoweko katika Jimbo la Manonga yapo ndani ya Mbuga ya Wembere ambayo kwa sasa imekosa sifa ya kuwa hifadhi ya wanyama na wananchi katika Kata hizo wameongezeka na kufanya kukosekana kwa maeneo ya makazi, kilimo na ufugaji na kwa kutokuwepo mipango mizuri ya matumizi bora ya ardhi kwa sababu ya hifadhi hiyo na kusababisha migogoro mikubwa kati ya wakulima na wafugaji na kuleta mauaji:-


Je, ni lini Serikali italitenga na kulipima eneo la Hifadhi ya Wembere hususan katika maeneo ya Kata hizo kwa ajili ya matumizi bora ya ardhi?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa Pori Tengefu Wembere, Serikali inakusudia kulibadilisha hadhi pori hili kuwa Pori la Akiba. Katika zoezi hili alama za mipaka ya hifadhi na maeneo yanayopakana zitapitiwa na kuhakikiwa upya.

Mheshimiwa Spika, aidha, mipango ya matumizi bora ya ardhi hufanyika katika maeneo ya vijiji na husimamiwa na Wizara za Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Wizara yangu iko tayari kushirikiana na mamlaka hizi na wadau wengine pale itakapohitajika.

Mheshimiwa Spika, mbuga ya Wembere ina ukumbwa wa kilimeta za mraba 8,784 na ilitambuliwa kisheria kuwa Pori Tengefu kwa Tangazo la Serikali Na. 269 la mwaka 1974, pori linapatikana katika Mikoa ya Singida (Wilaya ya Manyoni) na Mkoa wa Tabora (Wilaya za Igunga, Sikonge na Uyui).

Mheshimiwa Spika, Pori Tengefu Wembere ni ardhi oevu (Chepechepe) ambayo ni muhimu Kitaifa na Kimataifa kwa kuwa ni chanzo cha maji dakio na chujuo la maji ya Ziwa Kitangiri na Eyasi. Pori hili ni mazalia na ushoroba wa wanyamapori ambao ni kiunganishi pekee cha mfumo wa ikolojia wa Hifadhi za Taifa ya Ruaha na Serengeti, mapori ya akiba ya Rungwe, Kizigo, Muhezi na Ugalla. Aidha, pori ni makazi na mazalia ya ndege wahamao ambapo mwaka 2001 utafiti wa Kimataifa ulibaini uwepo wa zaidi ya spishi 12 za ndege walio hatarini kutoweka.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa, pori hili linatumika kwa uwindaji wa kitalii na utalii wa picha ambapo fedha inayopatikana hutumika kwa ajili ya uboreshaji wa huduma za jamii kupitia Halmashauri za Wilaya husika.